|
Amesema Ibn
Sa’ad - Allah amrehemu: “Mtume wa Allah alimtuma huru wake Zayd Ibn
Haarithah na Abuu Raafii kwenda mjini Makkah kuwahamisha Ahli zake na
akawapa ngamia wawili na Dir-ham mia tano (500) ziwasaidie safarini.
(Wakarudi Madinah) na kumletea Fatma na Umuu kulthuum binti za Mtume wa
Allah, na Bi. Saudah Bint Zum-ah mkewe (mtume). Ama Bi Rukia (Bint
mwingine wa Mtume) yeye alikwa amekwisha hama zamani pamoja na mumewe:
Uthman Ibn Affaan. Bi Zainab (bint ya Mtume )nae alizuiliwa na mumewe
Abul-aaswi Ibn Ar-rabii kuondoka. Zayd Ibn Haarithah akamchukua mkewe,
Umuu Ayman pamoja na mwanawe Usaamah. Abadallah Ibn Abuu Bakri ndiye
aliyeondoka na watu hawa pamoja na familia ya Abuu Bakri akiwemo pia Bi.
Aysha kuja Madinah. Akafikia nao katika nyuma ya Bwana haarithah Ibn
An-numaan” Baada ya Ahulu Bayt na Mtume kuhama Madinah wakitokea Makkah
ambako usalama wao ulikuwa hatarini. Mtume - Rehema na Amani zimshukie -
aliendelea na shughuli yake aliyokuwa ameianza akiwa kama Mtume wa Allah
na kiongozi wa mji huo wa madinah. Aliendelea kuratibu masuala yake na ya
jamii ya maswahaba wake ili kuasisi jamii njema itakayopigiwa mfano kwa
kila jambo jema. Jamii itakayojengwa katika misingi ya upendo, udugu,
uadilifu, usawa, kusaidiana na kujitoa muhanga kwa jaili ya manufaa ya
umma. Hii ndio misingi na nguzo imara za jamii njema iliyowekwa na mfumo
sahihi wa maisha, uislamu ili jamii ya wanadamu mahala popote ilipo na
zama zozote iwazo iweze
kuishi ikiwa kama ndugu moja yenye kusaidiana ikitawaliwa na
mshikamano wa kidungu na kufunikwa na wingu la amani na salama. Hii ndio
iliyokuwa sera na siasa aliyoitumia Mtume wa Allah- Rehema na Amani
zimshukie ili kuhakikisha kuwa anaasisi jamii njema, yenye utu kamili:
‘NA SHIKAMANANENI KWA KAMBA (dini) YA ALLAH NYOTE, WALA MSIACHANE. NA
KUMBUKENI NEEMA YA ALLAH ILIYO JUU YENU., (zamani) MLIKUWA MAADUI, NAYE
AKAZIUNGANISHA NYOYO ZENU, HIVYO, KWA NEEMA YAKE, MKAWA
NDUGU………………………..(3: 103).
SOMO LA TATU
i.
ATHARI ZA HIJRAH KWA WATU WA MADINAH.
MADINAH YAANZA
UKURASA MPYA WA MAISHA, MAISHA YA AMANI NA UTULIVU BADALA YA MAISHA YA
VITA NA UADUI.
Mji wa Madinah
(Yathrib) ulikuwa ukikaliwa na watu wenye asili tofauti waliosheheni chuki
za ukabila, wenye itikadi tofauti, kila kundi likijiona bora kuliko
jingine. Kila kundi likitumia nguvu na rasilimali zote kuhakikisha kuwa
linakuwa bwana na mtawala wa makundi mengine. Mayahudi “Ahlul-Kitaab”
walikuwa ni sehemu ya jamii ya wakazi wa Madinah. Jamii ya mayahudi wa
madinah iliundwa na makabila matatu, Baniy Nadhwiyr, Baniy Quraydhwah na
Baniy Qayunqaa, kila kabila likiwa limegawanyika
katika koo kadhaa. Hawa ndio waliokuwa wakitawala kwa miongo kadhaa uchumi
wa mji wa Madinah. Walishika hatamu katika nyanja za kilimo na biashara.
Jamii nyingine ya wakazi wa Madinah, ilikuwa ni jamii ya Waarabu
washirikina iliyoundwa na makabila mawili makuu, Ausi na Khazraj ambayo
pia yalikuwa yanaundwa na koo kadhaa. Historia inaonyesha kwamba waarabu
hawa walifika madinah mwishoni mwa karne ya nne (4) ya Miladia (4th
C A.D) wakitokea nchini Yemen. Kwa kiasi kikubwa ustadi wa kilimo
waliokuwa nao Mayahudi walijifunza kutoka kwa waarabu hawa. Makundi haya
mawili, Mayahudi na Waarabu hayakuwa na mafungamano mazuri baina yao. Bali
ndani ya makundi haya pia hakukuwepo masikilizano na maelewano baina ya
wenyewe kwa wenyewe. Waarabu waligawika katika makundi pinzani kama
ilivyokuwa kwa upande wa Mayahudi pia. Moto wa uadui na chuki baina ya
kundi na kundi ulikuwa ukiwaka mara kwa mara katika mji wa Madinah.
Ushindani na ugombeaji wa maslahi ndio uliokuwa kwa kiasi kikubwa mafuta
na kuni za moto huu uliokuwa ukiziangamiza na kuzivuna roho za wakazi wa
Madinah. Ausi na Khazraj walipofikishwa bidhaa adimu, ghali, yenye faida
kubwa, yaani ujumbe wa Uislamu, dini pekee iliyoridhiwa na Allah kwa
wanadamu wote “……………….NA NIMEKUPENDELEENI (nimekuridhieni)
UISLAMU UWE DINI YENU…………….” 5: 3
“BILA SHAKA
DINI (ya haki )MBELE YA ALLAH NI UISLAMU………” (3: 19)
wakakubali
kuinunua bidhaa hii kwa
thamani ya mali na nafsi zao: “ALLAH AMENUNUA KWA WAUMINI NAFSI ZAO NA
MALI ZAO( wote nafsi na mali zao katika kupigania dini hii) ILI NA YEYE
AWAPE PEPO. WANAPIGANA KATIKA NJIA YA ALLAH, WANAUA NA WANAUAWA
…………..” (9: 111)
wakasilimu na
kuwa waislamu wa kweli, wanyenyekevu na watiifu kwa Allah na Mtume wake,
wakiliitikia agizo la Mola Wao. :” ENYI MLIOAMINI! MTIINI ALLAH NA MTUME
WAKE NA WENYE MAMLAKA JUU YENU, WALIO
KATIKA NYIE (waislamu wenzenu)………….” (4: 59)
hawa kwa pamoja
wakaunda kundi lenye nguvu itokanayo na imani ya kweli, kundi la Answaar
alilolitaja Allah ndani ya kitabu chake kitukufu: “ ………….NA WALE
WALIOWAPA (Muhajiri) MAHALA PA KUKAA ( nao ni Answaar) NA WAKAINUSURU
(dini ya Allah, ) HAO NDIO MARAFIKI, WAO KWA WAO……………” (8:
72).
Kundi hili
likazidi kuimarika zaidi pale ndugu zao Muhajirina waislamu makurayshi
walipojiunga nao kama wakimbizi wa Imani kutoka Makkah. Hawa ndio
wanaotarajwa na kauli ya Allah: “ HAKIKA WALE WALIOAMINI NA WAKAHAMA NA
WAKAPIGANIA DINI YA ALLAH KWA MALI ZAO NA NAFSI ZAO…………..’ (8:
72).
Hili likawa ni
kundi jipya kuzaliwa katika jamii ya
wakazi wa Madihan, kundi la waislamu. Kundi hili likaigeuza kabisa sura
yakisiasa ya Madina. Madinah sasa ikawa ni ya makundi mawili, kundi la
haki (waislamu) na kundi la batili (mayahudi - mushrikina). Kundi la haki
likitazamwa na makafiri kama adui mkubwa. “HAKIKA UTAWAKUTA WALIO MAADUI
ZAIDI KULIKO WATU(wengine) KWA WAISLAMU NI MAYAHUDI NA WALE MUSHRIKINA
(Wasiokuwa na kitabu)…………..”
(5: 82)
Hivi ndivyo
Mtume wa Allah - Rehema na Amani zimshukie alivyoukuta mji wa Madinah
ukiwa na mchanganyiko wa makundi na itikadi tofauti za kishirikina.
Makundi ambayo hayafungamanishwi na nidhamu (utaratibu/mpango) moja
ya maisha, hayana umoja wala mshikamano. Bwana Mtume akaiona hatari ya
mchanganyiko huu wa imani potofu, chuki za kikabila na ugombeaji wa
madaraka, hapa ndio pakawa mahala pa kuanzia. Mjumbe wa Allah akafanya
kazi na juhudi kubwa katika kuibadilisha jamii hii kutoka katika mfumo
mbaya na mbovu wa maisha kuipeleka katika mfumo shaihi wa maisha, wenye
amani waliochaguliwa na Mola Muumba wao. Akapanga mikakati ya kuiunganisha
jamii ile iliyogawanyika katika misingi ya ukabila na kuikusanya pamoja
dini ya chuo kikuu cha utu. Akaasisi moyo wa kushirikiana na kusaidiana
katika misingi ya udugu wa kiislamu ambao huwafanya waislamu kuwa ndugu
moja: “ KWA HAKIKA WAISLAMU WOTE NI NDUGU………” (49: 10)
Udugu huu
uliimarishwa zaidi na uhusiano alioujenga, uhusiano baina ya muislamu na
Muumba wake, uhusiano baina ya muislamu na muislmau mwenziwe na uhusiano
baina ya muislamu na asiye muislamu.`
a./. UHUSIANO
BAINA YA MUISLAMU NA ALLAH.
Uhusiano
huu baina ya mja na Mola wake ulijengwa katika misingi ya kumuabudu
yeye pekee bila ya kumshirikisha na chochote kiwacho.
“MWABUDUNI
ALLAH WALA MSIMSHIRIKISHE NA CHOCHOTE…….” (4: 36) juu ya itikadi ya
kuwa YEYE ALLAH ndiye Bwana Mlezi wa viumbe vyote: “SHUKRANI ZOTE
ANASTAHIKI ALLAH, MOLA WA WALIMWENGU WOTE” (1:2)
“……………….BWANA
MWENYE KUWALEA. MFALME WA WATU. MUABUDIWA WA WATU”
(114: 1-3)
waitakidi kwamba
Allah ndiye muumba anayeruzuku, anayehuyisha na kufisha. Ni yeye pekee tu
anayeweze kudhuru na kunufaisha na ni yeye pekee anayestahili kuabudiwa,
kunyenyekewa na kuombwa msaada na wafanye amali zao zote kwa ajili ya
kutaraji radhi zake tu.
b./. UHUSIANO
BAINA YA MUISLAMU NA NDUGUYE MUISLAMU.
Msingi wa
uhusiano huu ni udugu na kiimani ambao
Bwana Mtume aliufanya kuwa juu ya udugu wa nasabu/damu, akimtegemezea
kauli ya Allah: KWA HAKIKA WAISLAMU WOTE NI NDUGU…………….’ Naye
Mtume akaifasiri kauli hii ya Mola wake kwa kusema: “Muislamu ni ndugu
ya Muislamu, hamdhulumu na wala hamsalimishi (kwa makafiri). Na
atakayemsaidia nduguye naye atapata msaada wa Allah, na atakayemuondoshea
muislamu mwenziwe matatizo
(shida), Allah atamuondoshea mtu huyo matatizo/shida miongoni, mwa
matatizo ya siku ya kiyama. Na mwenye kumsitiri muislamu mwenziwe naye
atasitiriwa na Allah siku ya Kiyama”Bukhaariy na Muslim.
Ni kutokana na
msingi huu ndio Bwana Mtume Rehema na Amani zimshukie akaunga udugu baina
ya Muhajirina (wakimbizi wa Imani) na Answaar (wasaidizi/watetezi wa
imani). Kila muhajiri awa na nduguye wa imani Muanswaar. Muanswaar
akagawana mali, nyumba na shamba na nduguye muhajiri nusu bin nusu. Undugu
huu ukawafikisha mahala pa muanswaar kuwa tayari taliki mmoja wa wakeze
ili aolewe na nduguye Muhajiri kama alivyofanya hivyo Sa’ad Ibn Rabii
(Muanswaar) kwa nduguye Muhajir, Abdul-Rahman Ibn Auf. Answaar wakapiga
mfano wa udugu uiso na mithili katika historia nzima ya mwanadamu, huu
ndio udugu anaoutaja Allah ndani ya kitabu chake kitukufu. “ NA WALE
WALIOFANYA MASKANI YAO HAPA (yaani madinah) NA WAKAUTAKASA UISLAMU (wao
barabara) KABLA YA (kuja) HAO (Muhajiri huko Madinah) NA WAKAWAPENDA HAO
WALIOHAMIA KWAO, WALA HAWAPATI, HAWAONI DHIKI NYOYONI MWAO KWA HAYO
WALIYOPEWA (hao Muhajiri) NA WANAWAPENDELEA KULIKO NAFSI ZAO INGAWA
WENYEWE WANA HALI NDOGO……………” 59:9)
Udugu huu
ukakata kabisa mizizi ya ubaguzi na tofauti katika misingi ya ukabila,
nasabu, rangi na utaifa. Hii ni aina pekee ya udugu katika historia ya
jamii ya wanadamu.
c./. UHUSIANO
BAINA YA MUISLAMU NA ASIYE MUISLAMU.
Mtume wa Allah
Rehema na Amani zimshukie hakufanya kosa la kuitenga na kuibagua jamii ya
wasiokuwa waislamu. Bali alihakikisha kuwa kunakuwepo mafungamano na
uhusiano usio na madhara baina ya waislamu na wasio waislamu (Mayahudi).
Uhusiano huu aliujenga katika misingi ya ubinadamu ambao
unamuunga na kumjumuisha pamoja bianamu na binadamu mwenzie. Mizani
ya udugu huu ikawa ni kauli yake Mtume: “Wapendelee watu uyapendayo
wewe”.Bukhaariy.
Hii ni kutokana
na kutambua kwake Bwana Mtume kwamba watu pamoja na tofauti ya jinsia na
itikadi zao, wanategemeana katika haja zao mbalimbali za kimaisha ya siku
hata siku. Kwa hivyo ni lazima wawe pamoja, washirikiane na wasaidiane. Na
hapana njia ya kusaidiana na kushirikiana ila chini ya njia ya mwavuli
salama, amani na utulivu. Na amani na utulivu havitapatikana mpaka jamii
ya wanadamu itawaliwe na hisia za udugu upendo na mafungamano ya
kibinadamu. Chini ya hisia hizi kila mtu ataheshimu utu, hadhi na itikadi
ya mwenziwe. Ili kuonyesha kuwa Mtume wa Allah anajali na kuthamini utu,
heshima na imani ya watu wengine aliandikiana mkataba na Mayahudi. Mkataba
huu uliwapa Mayahudi uhuru kamali wa kuabudu kwa mujibu wa itikadi yao.
Waislamu na Mayahudi wawe kitu kimoja dhidi ya adui yeyote
atakayeishambulia Madinah. Mtu yoyote, muislamu au muyahudi ana haki ya
ama kuishi Madinah au kokote kule akutakako.
|