|
III/. QUR-ANI YAWATETEA WAUMINI.
Hali ilipofikia hatua hiyo ndipo ulipokuja uokovu na msaada
kutoka mbinguni. Wahyi ukamshukia Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-kwa
kauli yake Allah Mola Mtukufu: “WANAKUULIZA (hukumu ya) KUPIGANA VITA KATIKA
MIEZI MITAKATIFU. SEMA: KUPIGANA VITA KATIKA (miezi) HIYO NI DHAMBI KUBWA. NA
KUWAZUILIA WATU NA DINI YA ALLAH, NA KUMKANUSHA (Allah), NA (kuwazuilia watu)
MSIKITI HUO MTAKATIFU, NA KUWATOA HUMO WATU WALIOMO, NI (dhambi) KUBWA ZAIDI
MBELE YA ALLAH. NA KUWAZUILIA WATU NA DINI YAO NI MBAYA ZAIDI KULIKO KUUA.
WALA HAWATAACHA KUPIGANA NANYI MPAKA WAKUTOENI KATIKA DINI YENU, KAMA
WAKIWEZA. NA WATAKAOTOKA KATIKA DINI YAO KATIKA NYINYI, KISHA WAKAFA HALI YA
KUWA MAKAFIRI, BASI HAO NDIO AMALI ZAO ZIMEHARIBIKA KATIKA DUNIA NA AKHERA. NA
NDIO WATU WA MOTONI, HUMO WATAKAA MILELE”. [2:217]
Naam, ni kweli na sio uongo kwamba kupigana vita katika miezi
mitakatifu ni dhambi kubwa. Lakini kitendo kilichofanywa na mushrikina ni
dhambi na hatia kubwa zaidi. Wao waliikanusha na kuipinga dini ya haki,
wakawazulia watu na dini hiyo ya haki na isitoshe wakavunja utukufu wa mji
wenye amani (Makkah). Wakawaudhi waislamu kwa kila aina ya maudhi na
adhabu/mateso mpaka wakafitinika na dini yao waliofitinika. Na wakafa
waliokufa kutokana na adhabu kali waliyoipata. Wakakimbia kwa ajili ya dini
yao waliokimbia huku wakiwaacha nyuma wake, watoto, wazazi, ndugu, jamaa na
mali zao. Wakawatoa katika mji na majumba yao pasina haki bali kwa dhuluma tu.
Na wakaweka pingamizi baina ya waislamu na msikiti mtukufu na ilhali wao
waislamu ni wenyeji na walinzi wa msikiti huo. Kisha makafiri hawa wakaendelea
kuwafukuza waumini kila wanapokimbilia wakiwashakizia maadui na kuchochea
fitina dhidi yao. Wakaendelea kuwaendea nyendo za kedi na vitimbi mpaka
wawamalize au wawatoe katika dini yao na kuwarejesha ukafirini. Basi je, ni
dhambi ipi iliyo kubwa zaidi kuliko kumzuiia mtu na dini yake? Na je, ni
khasara ipi iliyo kubwa zaidi kuliko mtu kurejea ukafirini baada ya kuamini?
Kurejea upotevuni baada ya uongofu? Kurejea vizani baada ya kuwa nuruni?
Makurayshi waliwatendea waislamu vitendo vingi vibaya lakini
wakajisahaulisha hayo yote. Wasikumbuke ila tu tukio hili la kuuawa kwa Ibn
Al-Hadhwramiy na kutekwa kwa msafara wao. Wakalifanya tukio hili kuwa ni hoja
dhidi ya Mtume wa Allah, wakiitumia hoja yao hiyo kupandisha mori wa Waarabu
dhidi ya Waislamu na Uislamu. Lakini Allah Mola Mjuzi wa yote aliwafunga
vinywa vyao na akawakinga waislamu na vitimbi vyao. Na akalifanya tukio hili
kuwa ni ufunguo wa ukurasa wa kheri na sababu ya nusura (ushindi) na msaada
walioupata waislamu katika vita vya Badri.
Ibn Is-haaq-Allah amrehemu-anasema: “Qur-ani iliposhuka na
kadhia hii, na Allah akawafariji waislamu kutoka katika hali ya ukungu
waliyokuwemo. Hapo ndipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaupokea
msafara na wale mateka wawili. Makurayshi wakatuma ujumbe kutaka kuwakomboa;
Uthman Ibn Abdillah na Al-Hakam Ibn Kiysaan kwa kutoa fidia. Mtume wa Allah
akawaambia (wajumbe waliotumwa): “Hatupokei fidia yenu mpaka warudi wenzetu
(yaani Sa’ad Ibn Abiy Waqaasw na Utbah Ibn Ghaz-waan), kwani sisi
tunakucheleeni juu yao. Mkiwauwa nasi tutawaua wenzenu hawa”. Sa’ad na
Utbah wakarudi, hapo Mtume wa Allah akapokea fidia na kuwaachia makurayshi
wale”.
Suala la Abdullah Ibn Jahshi na wenzake lilipopata ufumbuzi
kutoka mbinguni kwa kushuka Qur-ani, walitumai kupata ujira, wakasema: Ewe
Mtume wa Allah, tunatumai kuwa sisi ni wapiganaji tunaostahiki kupewa ujira wa
mujahidina. Allah akashusha kwa ajili yao: “HAKIKA WALE WALIOAMINI NA WALE
WALIOHAJIRI (wakahamia Madinah) NA WAKAPIGANA KATIKA NJIA YA ALLAH. HAO NDIO
WANAOTUMAI REHEMA YA ALLAH NA ALLAH NI MWINGI WA KUSAMEHE (na) MWINGI WA
KUREHEMU”. [2:218]
UTETEZI HUU WA ALLAH ULIWASHAJIISHA WAISLAMU KUENDELEA KUTOA
UPINZANI KWA MAKURAYSHI.
Allah Mola Mwenyezi akawabainishia watu kwamba vitendo
walivyovifanya makurayshi kuwafanyia waislamu vilikuwa ni vibaya zaidi.
Ukilinganisha na kitendo hiki walichokifanya waislamu cha kuua katika mwezi
mtukufu. Utetezi huu wa Allah kwa kitendo kilichofanywa na Abdullah na wenzake
na kuwatumainiza msamaha na rehema yake. Uliwashajiisha waislamu kuendelea
kupambana na makurayshi. Mapambano na upinzani huu vilikuwa ni onyo kali kwa
kila anayeushambulia Uislamu na waislamu. Kwamba anayefanya hivyo ajue wazi
kuwa yatamfika yanayowafika makurayshi hivi sasa. Waumini nao kwa upande wao
wakatambua kuwa sasa wamo katika hatua (kipindi) mpya ya mapambano. Kwa hivyo
ni wajibu wao kujiandaa na kipindi hiki kwa nguvu zao zote. Na wakajua kwamba
wao hawana hatia ya kuua pale watakapomuua yule anayewafitinisha na kuwazuilia
na dini yao, hata kama ni katika miezi mitukufu: “MWEZI MTAKATIFU KWA MWEZI
MTAKATIFU, NA VITU VITAKATIFU VIMEWEKEWA KISASI (vikiondolewa hishima yake).
NA WANAOKUSHAMBULIENI, NANYI PIA WASHAMBULIENI KWA KADRI WALIVYOKUSHAMBULIENI.
NA MUOGOPENI ALLAH (msiongeze kuliko walivyokufanyieni) NA JUENI KWAMBA ALLAH
YU PAMOJA NA WANAOMUOGOPA”. [2:194]
Hapa sasa ndipo makurayshi walipodiriki kwamba kumbe
yawakutayo sasa ni kulipia matendo yao maovu waliyowatendea waislamu. Na
kwamba sasa waislamu ni ngangari hawatakubali kuonewa na kudhulumiwa tena.
Wakapata hisia kwamba waislamu hawa waliokuwa madhalili na wanyonge jana. Leo
wamekuwa na nguvu kiasi cha kuwa ni kikwazo na tishio kwa misafara yao ya
kibiashara kwenda na kutoka Shamu. Makurayshi wakaanza kuutazama upya mtazamo
wao kuelekea waislamu na kutumia muda mwingi kupanga mikakati ya kuihami
misafara yao. Wakati makurayshi wakifikiria jinsi ya kuihami misafara yao,
waislamu nao kwa upande wao walikuwa wakipanga mikakati ya kuiteka misafara
hiyo. Ni vema ikaeleweka kwamba misafara hii ya biashara ndio iliyokuwa uti wa
mgongo na chimbuko la nguvu za kiuchumi za makurayshi. Faida iliyopatikana
kutokana na biashara hii ndio iliyowapa nguvu na jeuri ya ukandamizaji
sambamba na matumizi ya mabavu. Waislamu wakakusudia kuuvunja uti huu wa
mgongo wa uchumi wa makurayshi ili kuwadhoofisha kiuchumi na kijeshi.
|