Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

III) WAZAZI WA MTUME NA KISA CHA KUCHINJWA KWAKE ABDALLAH

 

Tumeeleza katika somo lililopita kwamba baba yake Bwana Mtume ni Mzee Abdallah Bin Abdul-Mutwalib na mama yake ni Bi Aaminah Bint Wahab. Bwana Abdallah alikuwa ni miongoni mwa vijana bora wa mji wa Makkah na alikuwa mzuri wa umbo na tabia njema. Bi Aaminah alitokana na kabila tukufu na alikuwa ni miongoni mwa mabinti wa makkah waliosifika kwa tabia njema na alijaaliwa na umbo na sura nzuri.

Baada ya Bwana Abdallah kumuoa Bi. Aaminah alisafiri pamoja na mkewe kuelekea Shaamu kwa ajili ya biashara,Wakati anarudi Makkah akitokea Shaamu alishikwa na maradhi njiani, akaamua kwenda kujitibia Madinah ambako maradhi yalimzidia akafa na kuzikwa hapo hapo Madinah.

Baada ya mazishi mkewe alirudi Makkah hali ya kuwa ana huzuni ya kumpoteza mumewe mpenzi na wakati huo Bin. Aaminah alikuwa na mimba ya Bwana Mtume

Ama kisa cha kuchinjwa Bwana Abdallaha baba yake Mtume kilikuwa kama ifuatavyo:-

Bwana Abdallah alikuwa akipendwa sana na baba yake kuliko nduguze wengine. Ikatokezea kukauka chem chem ya maji ya ZamZam nyakati za Hijjah ndipo Mzee Abdul- Mutwalib akaweka nadhiri ya kumchinja mmojawapo wa wanawe kwa ajili ya kujikurubisha kwa Mola wake maji yatakapozidi/yatakapoongezeka. Maji yalipoongezeka ndipo ikamlazimu Bwana Abdallah kuitekeleza nadhiri aliyoiweka ya kumchinja mmojawapo wa wanawe. Sasa achinjwe nani? Ikabidi ipigwe kura, na kila mara ikawa inamuangukia Bwana Abdallah baba yake Mtume.

Kwa kuwa mtoto huyu ndiye aliyekuwa kipenzi cha baba yake bali watu wote ndipo kiongozi mmoja wa dini akamshauri Mzee Abdul-Mutwalib apige kura baina ya mwanawe Abdallah na idadi fulani ya ngamia. Kila mara kura itakapo muangukia Abdallah iliongezwa idadi ya ngamia mpaka kura iwaangukie ngamia. Idadi ya ngamia ilipofika ngamia mia ndipo kura ikawaangukia ngamia wale, Mzee Abdul-Mutwalib akawachinja ngamia wale kwa ajili ya kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu na kwa kitendo hicho ikawa Bwana Abdallah ameokoka na kuchinjwa na ngamia wale wakawa ndio fidia yake. Kisa hiki kinatukumbusha kisa kikongwe kilichojaa mafunzo mengi cha kutaka kuchinjwa Nabii Ismail Bin Ibrahim – Amani ya Allah iwashukie wakati Nabii Ibrahim alipooteshwa usingizini amchinje mwanawe Ismail. Kwa kuwa ndoto za mitume huwa ni wahyi kwa Mwenyezi Mungu, Nabii ibrahim akaanza kuchukua hatua za kuitekeleza amri ya Mola wake, akamlaza mwanawe ili amchinje ndipo Mola mwingi wa huruma akamkomboa mja wake Ismail kwa kumleta kondoo wa peponi achinjwe badala ya Ismail kama tunavyosoma ndani ya Qur-ani.

Imepokelewa hadithi kutoka kwa Bwana Mtume akisema: "Mimi ni mtoto wa wachinjwa wawili " Nao ni Babu Nabii Ismail, huyu ndiyo mchinjwa wa kwanza na wa pili ni baba yake Mzee Abdallah.

 

SOMO LA NNE

i/ KUZALIWA KWA BWANA MTUME

Bwana Mtume – Allah amshushie rehma na amani – alizaliwa katika mji wa Makkah, siku ya Jumatatu mwezi wa mfungo sita, mwaka wa tembo sawa na tarehe 20 ya mwezi April mwaka 571 – Miyladia (tangu kuzaliwa Nabii Issa). Bwana Mtume alizaliwa hali ya kuwa ni yatima kwani baba yake alikufa akimuacha mkewe ana mimba ya Mtume. Mama yake alipojifungua tu alimpeleka mjumbe kwa babu yake Mtume Mzee Abdul -Mutwalib kumpa khabari njema za kuzaliwa mjukuu wake. Mzee Abdul – Mutwalib akafurahikia sana mjukuu wake akamchukua na kumzungusha katika Al-Kaaba na akamuita Muhammad.

Tumesema Bwana Mtume amezaliwa mwaka wa tembo. Qur-ani Tukufu imeuzungumza mwaka huu katika sura maalum iliyoitwa kwa jina la Suuratul –Fiyl (Sura ya tembo) kisa cha mwaka wa tembo kinaanzia pale Abraha mfalme wa Habashah na Yaman alipowaona Waarabu wakihiji Makkah na ibada hii ya Hijjah ikaufanya mji wa Makkah kuwa ni kitovu cha biashara . Mfalme Abraha akadhamiria kuihamisha ibada hii ya Hijjah kutoka Makkah na kuipeleka katika milki ya himaya yake ya Yaman. Ili kuutekeleza mkakati wake huu akajenga kanisa kubwa sana na kulipamba kwa mapambo ya fakhari ili watu wavutike na kuja kufanya ibada ya Hijjah hapo. Baada ya ujenzi huo, akawaamrisha watu waje kuhiji hapo, amri hii ikawa nzito kwa Waarabu kuitekeleza na hawakuiridhia. Ili kuonyesha chuki yao dhidi ya amri hii alitoka mtu mmoja wa kabila ya kinaanah akaja kufanya haja kubwa ndani ya kanisa lile. Kitendo hiki cha kulichafua kanisa kilimkasirisha sana Mfalme Abraha, hasa baada ya kugundua kwamba mhusika wa kitendo hicho ni mtu kutokea pande za Makkah. Akaandaa jeshi kubwa lililokuwa limesheheni tembo wengi ili kwenda kuivunja Al-kaaba na yeye mwenyewe alikuwa amempanda tembo mkubwa sana kuliko wote. Waarabu wa Makkah waliogofya sana na jeshi lile. Jeshi la Abraha lilipofika katika viunga vya mji wa Makkah likawakuta ngamia, kondoo na mbuzi wa watu wa Makkah na wengine walikuwa ni milki ya babu yake Mtume Mzee Abdul-Mutwalib, Abraha awachukua wanyama wale wote. Mzee Abdul-Mutwalib kiongozi wa kabila la Kikurayshi, mtumishi wa Al-Kaab na mtawala wa Makkah akamuendea Abraha na kumtaka amrejeshee wanyama wake aliowachukua Abraha akamshangaa sana Mzee Abdul – Mutwalib akamwambia:

"Mimi nilitazamia umekuja kuniomba nisiivunje Al-Kaab, kumbe umekuja kunitaka nikurudishie wanyama wako!" Mzee Abdul – Mutwalib akamjibu: "Mimi wa kwangu ni hawa wanyama, ama hii nyumba yupo mwenyewe atayeihami".

Kisha Mwenyezi Mungu Mtukufu alishushia jeshi la Abraha jeshi la ndege wanaolidondoshea jeshi la Abraha mawe kutoka motoni. Jiwe likimpata mtu anasagikasagika yeye na tembo wake na kuwa kama majani yaliyoliwa na wadudu kama tunavyosoma ndani ya Qur-ani. Tokea hapo Waarabu wakawa wanaitaja kalenda yao kwakuinasibisha na tukio hili kubwa na hii ndio maana tunasema Bwana Mtume alizaliwa mwaka wa tembo.

 



Forum | Guestbook | Tuandikie |