|
i) MALEZI YA MTUME NA KIFO CHA MAMA YAKE :
Mtume alifiwa na baba yake kabla
hajazaliwa na hakumuachia mali ya kutosha. Mtume alipofikia umri wa miaka
minne, mlezi wake na mnyonyeshaji wake Bi Haliymah alimrejesha kwa mama yake
Bi Aaminah akamlea mwanawe mpaka alipofikia umri wa miaka sita akampeleka
kuwazuru wajomba zake Madinah. Bi Aminah alifia njiani wakati akirejea
Makkah wakati akirejea na mwanawe baada ya ziara yake ya Madinah na akazikwa
ABUWAI, kitongoji kilichoko baina ya Makkah na Madinah. Baada ya maziko ya
mama yake Mtume, Mtume alichukuliwa na kupelekwa Makkah UMMU AYMANA
muhabeshi. Huyu alikuwa ni mtumishi aliyeachwa na baba yake na ndiye
aliyefuatana na mama yake Mtume safarini.
Baada ya kufiwa na mama yake, Mtume
alilelewa na babu yake mzaa baba Mzee Abdul Mutwalib kwa kipindi
kisichopungua miaka miwili. Babu yake alimpenda sana mjukuu wake huyu kiasi
cha kumtanguliza kuliko wanawe (ami zake Mtume) na alikuwa akimketisha
mahala anapokaa yeye kwa kumtukuza. Mtume alipofikisha umri wa miaka minane,
babu yake alifariki dunia. Kabla hajafariki, alimuusia mwanawe Abuu Twalib
kumlea mjukuu wake, hivyo Mtume akawa chini ya uangalizi na ulezi wa Ammi
yake Bwana Abuu Twalib. Abuu Twalib alikuwa na mzigo wa familia kubwa na
alikuwa na mali kidogo tu ambayo haikumtosha kuihudumia familia, lakini
MwenyeziMungu akamkunjulia riziki yake kutokana na kumlea mtoto huyu yatima.
Mtume aliishi nyumbani kwa ammi yake kama mmoja wa watoto wa familia ile na
alikuwa akitosheka na alichopewa; hakuwa akililia na kupupia kila
alichokiona kama ilivyo tabia na ada ya watoto.
ii) SAFARI YA MTUME NA AMMI YAKE
KUELEKEA SHAMU
Bwana Mtume –Allah amshushie
rehema na amani- alipofikia umri wa miaka kumi na nane alisafiri pamoja na
ammi yake Abu Twalib kuelekea Shamu. Hii ilikuwa ni safari ya kibiashara.
Walipofika katika HUURAANA wakiwa njiani kuelekea BASRAH nchini Shamu, hapo
padri wa kiyahudi jina lake Bahiyrah alimuona Mtume akifunikwa na kiwingu
kutokana na jua kali la jangwani wakati msafara wao ulipokuwa unakaribia
hapo. Msafara ukaja ukapumzika chini ya mti uliokuwa jirani na kibanda cha
padri yule, padri akakiona kiwingu kimefunika mti ule waliopumzika chini
yake Mtume na watu wengine waliokuwemo katika msafara ule wa kibiashara,
akayaona matawi ya mti ule yamemuinamia kijana mmoja aliyekuwemo katika
msafara ule. Bahiyrah alikuwa mwanachuoni wa kiyahudi na alikuwa amesoma
katika TAURATI na INJILI juu ya Mtume atakayetokea Bara Arabu. Bahiyrah
akaandaa chakula na kuualika msafara mzima katika karamu nyumbani kwake
kinyume na ada yake, kwani hakuwa na tabia ya kuwaalika chakula watu
nyumbani kwake. Msafara ulipohudhuria karamu, Bahiyrah akawa anamkazia sana
macho Bwana Mtume na akiziangalia alama alizokuwa nazo Mtume mwilini mpaka
akafanikiwa kuuona muhuri wa utume ulokuwa baina ya mabega yake. Hapo ndipo
padri Bahiyrah akamuuliza Bwana Mtume juu ya hali na mambo yanayomtokea
akiwa yu macho au usingizini. Bwana Mtume akamueleza yote yanayomtokea bila
ya kuficha hata jambo moja, Bahiyrah akaona aliyoelezwa na Mtume ndio sifa
za Mtume aliyebashiriwa katika kitabu alichonacho yeye yaani Taurati.
Bahiyrah akatambua kijana huyu ndiye Mtume angojewaye, ndipo akauliza wageni
wake waalikwa khabari za kijana yule na amefuatana na nani katika msafara
ule. Wakamuelekeza kwa ammi yake Bwana Abuu Twalib akamwambia :
"Mrejeshe mwanao huyu Makkah usiende naye Shamu kwani mayahudi
watakapomuona na kumtambua ndiye Mtume angojewaye watamuua kutokana na chuki
ya kuhama utume kwao na kwenda kwa waarabu." Abuu Twalib akazisikiliza
nasaha za Bahiyrah na akarudi naye haraka Makkah
|