|
Historia inatuambia kuwa kazi ya mwanzo kabisa iliyofanywa na Bwana Mtume ilikuwa
ni uchungaji wa kondoo na mbuzi. Aliamua kufanya kazi hii ile aweze kupata pesa za
kujikimu mwenyewe na kumpunguzia Ami yake Abdul Mutwalib ukali wa maisha. Hivyo Mtume
Rehma na Amani zimshukie akaanza kuchunga kondoo na mbuzi wa watu wa Makkah
kwa ujira mdogo aliokuwa akipewa. Kituo cha kazi yake hii ilikuwa ni "Ajyaad";
hii ni jangwa lililokuwa nje kidogo ya mji wa Makkah, hapo ndipo alipokuwa akiwachunga
wanyama hao.
Mwenyezi Mungu Mtukufu ana hekima kubwa sana katika kuifanya shughuli hii ya
uchungaji kuwa ndio kazi ya mitume. Wanayaanza maisha yao kwa kuchunga wanyama na
kuyahitimisha kwa kuwachunga binadamu wenziwao. Amesimulia swahaba Jaabir bin Abdillah
Allah amuwie Radhi akisema : [Tulikuwa pamoja na Mtume Rehma na Amani
zimshukie tukichuma matunda ya mabivu ya mpili mpili tawa, akasema "Chumeni
(matunda) yaliyo meusi kwani ndiyo matamu zaidi, mimi nilikuwa nikiyachuma wakati
nilipokuwa ninachunga kondoo na mbuzi". Tukamuuliza : Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu
ulikuwa ukichunga kondoo na mbuzi ? Akajibu "Ndio na hakuna mtume yeyote ila
alichunga"]
Kwa hiyo uchungaji wa kondoo ni alama nyingine inayothibitisha utume wa Nabii
Muhammad. Mwenyezi Mungu amejaalia uchungaji wa wanyama kuwa ni chuo cha kutoa mafunzo ya
uchungaji na uongozi kwa mitume wake. Wakiweza kuwachunga kondoo na mbuzi ambao hawa ni
wanyama wanyonge zaidi kuliko wengine, nyoyo zao zitatawaliwa na huruma na upole. Wakifuzu
ma kuhitimu katika chuo hiki kinachotoa mafunzo ya uchungaji na uongozi, ndipo hupewa
shahada zao kwa kukabidhiwa jukumu gumu na zito la kuwachunga binadamu wenziwao. Kama
walivoweza kuwastahamilia wanyama ndivyo wanavyotakiwa kuwavumilia wanadamu wenzao wenye
tabia ngumu zilizosheheni ukukutavu wa moyo. Tunasoma ndani ya Qurani Tukufu juu ya ugumu
wa nyoyo : "KISHA NYOYO ZENU ZIKAWA NGUMU BAADA YA HAYO (yote); HATA ZIKAWA KAMA MAWE
AU NGUMU ZAIDI (kuliko mawe)
[2:74]
Ni watu kama hawa ndio ambao Bwana Mtume anapewa jukumu la kuwalea na kuwachunga.
Kwa kuwa alihitimu vema chuoni, alifaulu kuifanya kazi yake hii ngumu kwa ufanisi mkubwa,
ingawa ilimgharimu subira ya hali ya juu. Mwenyezi Mungu anamtunukia Mtume wake shahada ya
kufaulu, pale aliposema : "BASI KWA SABABU YA REHEMA ITOKAYO KWA ALLAH UMEKUWA LAINI
KWAO (Ewe Muhammad) NA KAMA UNGEKUWA MKALI NA MWENYE MOYO MGUMU BILA SHAKA WANGALIKUKIMBIA
(usingelimpata hata mtu mmoja)
." [3:159]
Hii ndiyo natija na matunda ya uchungaji wa wanyama na hiyo hekima yake kwa
mukhtasari.
SOMO LA SITA :
i) SAFARI YA PILI YA SHAMU
Bi Khadijah binti Khuwaylid, Bibi mkureshi alikuwa ni mwanamke mwenye tabia njema,
anayekubalika na kuheshimika katika jamii ya watu wa Makkah. Mbali na sifa hizi, Bibi huyu
alikuwa miongoni mwa matajiri wakubwa wa mji wa Makkah, alipenda sana kufanya biashara.
Kutokana na kuona mbali na upevu wa akili yake alikuwa akiizalisha mali yake kwa kuwaajiri
watu. Aliwapa mali wakaiuze kwa mkataba na kuwapa sehemu ya faida iliyopatikana.
Habari za tabia murua, uaminifu na ukweli wa Bwana Mtume Rehma na Amani
zimshukie zilipoyagonga masikio ya Bi Khadija; akajawa na raghba ya kutaka
kumuhusisha mtu huyu mwaminifu na mkweli katika biashara yake. Akamtumia salamu za kumuita
naye Bwana Mtume akaitikia mwito. Bi Khadijah akamueleza alilomuitia ya kwamba amfanyie
biashara naye atampa sehemu kubwa ya faida itakayopatikana. Bwana Mtume akakubali na mara
moja akaianza kazi yake hii mpya ya biashara badala ya ya ile kazi yake ya kwanza ya
uchungaji. Ikumbukwe wakati huo Mtume alikuwa na umri wa miaka ishirini na tano. Akatoka
kuelekea Shamu katika msafara wa biashara akiambatana na Bwana Maysarah, msaidizi
aliyepewa na Bi Khadijah. Wakafika Shamu, wakafanya biashara wa kuuza na kununua, wakapata
faida kubwa sana kuliko iliyokuwa ikipatikana huko nyuma. Bwana Maysarah alishuhudia
katika safari yake na Bwana Mtume tabia njema, ukweli na uaminifu wa Mtume na hivi ndivyo
vilivyokuwa vigezo vya ufanisi katika biashara yao. Kadhalika aliona miujiza mingi
iliyoonyesha kwamba Muhammad ndiye Mtume mtarajiwa aliyebashiriwa katika vitabu
vitakatifu. Miongoni mwa miujiza hiyo ni pale Bwana Mtume alipopumzika chini ya mti
uliokuwa karibu na kibanda cha Padri Nestori. Padri huyu baada ya kumuona Mtume amepumzika
chini ya mti ule akamuendea Maysarah na kumuuliza khabari za Mtume. Bwana Maysara
akamueleza Padri Nestori kila alilolijua juu ya Mtume kwa kulisikia ama kulishuhudia yeye
mwenyewe. Hapo ndipo Padri Nestori akamwambia Bwana Maysara : "Hajapumzika chini ya
mti huu ila ni Mtume (Kwani huu ni mti wa mitume) basi (nakuusia) uhiifadhi siri hii (ili
mayahudi wasimdhuru)". Pia Maysarah alikuona wakati wa jua kali la utosi kiwingu
kikimfunika Bwana Mtume kumkinga na jua.

ii) MTUME AMUOA BIBI KHADIJAH :
Mara tu baada ya Mtume kurudi kutoka Shamu aliiwasilisha mara moja faida kubwa
iliyopatikana kutokana na biashara kwa Bi Khadijah. Bi Khadijah aliifurahia sana faida
hiyo ambayo hakuwahi kuipata kutoka kwa watu wengine aliowaajiri kabla ya Mtume Muhammad.
Kwa kigezo hiki Bi Khadijah akazidi kuthibitisha khabari zilizomfikia juu ya uaminifu na
ukweli wa Nabii Muhammad, ukiachilia mbali yale aliyoelezwa na mtumishi wake Maysarah
ambaye alikuwa msaidizi wa Mtume katika safari yao ya Shamu. Sifa zote hizi njema
zikamteka Bi Khadijah na kujikuta akimpenda Mtume na kutamani awe na mume mwenye sifa
njema kama Nabii Muhammad. Akamtuma mshenga kwa Mtume amuelezee nia yake ya kutaka kuolewa
naye. Ni vema ikakumbukwa kwamba wakati huo Bi Khadijah alikuwa ana umri wa miaka arobaini
na Bwana Mtume alikuwa amefikia umri wa miaka ishirini na tano. Bwana Mtume kwa kuzingatia
utukufu, heshima na tabia njema za Bi Khadijah bila ya kusita akakubali kumuoa bibi huyu.
Ndipo tena mipango na taratibu za harusi zikaanza na hatimaye wawili hawa wakawa ni mke na
mume. Ndoa hii ilifungwa miezi miwili tangu Mtume kurejea kutoka Shamu. Bibi huyu ameishi
na Mtume kwa karibu robo karne yaani kipindi kisichopungua miaka ishirini tano. Kwa
kipindi hiki chote Mtume hakumuolea Bibi huyu mke mwenza, naye ndiye mkewe wa kwanza. Bi
Khadijah alimzalia Bwana Mtume watoto sita, wawili wa kiume nao ni Kasim na Abdallah na
wanne wa kike nao ni Zainabu, Rukia, Ummu Kulthum na Fatimah. Ama Ibrahimu, huyu alizaliwa
na Bi Mariah Mqibtwi wa Misri. Ni vema tukakumbuka kuwa Bi Khadijah kabla ya kuolewa na
Mtume alikuwa ameolewa na Bwana Abu Haalah ambaye alimfia. Hivi ndivyo Bwana Mtume
alivomuoa Bi Khadijah Allah amuwie Radhi mama yetu huyu-.
|