Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

III) MWENENDO NA SILKA YA MTUME KABLA YA KUPEWA UTUME

Faida

Bwana Mtume –Rehma na Amani zimshukie- alijulikana miongoni mwa jamii yake kwa sifa na tabia zake njema kama vile ukweli, uaminifu, haya, unyenyekevu na upole. Jamii yake ilimkubali na ikampa jina la MKWELI MUAMINIFU. Huu ulikuwa ndio umaarufu wake pale mjini Makkah na kwingineko. Jamaa zake na jamii nzima walimuheshimu na kumpenda kwa kuwa alikuwa ni mtu mwepesi kuzoeleka na alishirikiana katika kazi mbali mbali za maendeleo katika jamii yao. Kutokana na tabia njema hizi alizopambika nazo Bwana Mtume, watu walikuwa wakienda kuweka amana zao kwake. Waliamini kuwa nyumbani kwa Mtume ndio mahala salama pa kuweka amana zao ambapo wanaweza kuzipata wakati wowote wakizihitajia hata kama ni usiku.

Lakini pamoja na mapenzi na heshima aliyoivuna Mtume kutoka kwa jamii yake, ikiwa ni jazaa ya tuzo na tabia zake njema kwao bado alihisi dhiki ndani ya nafsi yake. Bwana Mtume hakuichukia jamii yake kama watu bali alikerwa na tabia zao mbaya na itikadi yao potofu ya ushirikina. Hili ndilo lililomsumbua na ili kuonyesha chuki yake dhidi ya tabia na itikadi potofu ya jamii yake, hakupata kushirikiana nao katika kunywa pombe hata mara moja kiasi cha kuwashangaza walio wengi kwani ulevi lilikuwa ni jambo la kawaida kwa jamii ile mbali ya kuwa ni fakhri. Kadhalika hakuhudhuria hata mara moja sherehe na ibada za miungu sanamu japokuwa jamii yake ilimsihi sana ashirikiane nao lakini alikataa. Haya yote hayakuwa ila ni kwa fadhila zake Mwenyezi Mungu ambaye ndiye aliyemuhifadhi Mtume wake kutokana na uchafu ule wa kijahili. Kwa mukhtasari hivyo ndivyo Mtume alivyoishi na jamii yake kabla hajakabidhiwa rasmi dhamana ya Utume.

SOMO LA SABA

i) UFUMBUZI WA MTUME KATIKA MZOZO WA UWEKAJI WA “HAJAR ASWAD”

Watu wa Makkah walipoona kwamba jengo la nyumba ya Mwenyezi Mungu “Al-Kaaba” limeanza kuonyesha nyufa na kubomoka, viongozi wao waliona kuna umuhimu wa kuibomoa nyumba hiyo na kuijenga upya. Hivyo basi likapitishwa azimio la ujenzi wa “Al-Kaaba” katika kikao chao na ndipo mikakati ya ujenzi ilipoanza. Kila kabila likapewa jukumu lake katika kazi ile tukufu ya ujenzi wa nyumba tukufu ya Mtukufu Mwenyezi Mungu. Bwana Mtume nae hakubakia nyuma bali alishirikiana bega kwa bega na jamaa zake katika kazi ile tukufu ya ujenzi akibeba mawe mabegani pamoja nao.

Jengo lilipomalizika na kufikia hatua ya kuliweka “Hajar Aswad” {Jiwe Jeusi} mahala pake hapo ndipo ulipoanza mzozo wa nani apewe heshima na nafasi ya kuliweka jiwe lile tukufu mahala pake huku kila kabila likigombea nafasi hiyo na kujiona lina haki zaidi kuliko kabila jingine. Mzozo huu ulikuwa mkubwa sana kiasi cha kuhatarisha hali ya amani na utulivu waliyokuwa nayo kwa kukurubia kulipuka vita baina yao. Viongozi wao wenye busara waliona ni vema wakaketi chini kuutafutia ufumbuzi mzozo ule mbaya. Ni vema ikumbukwe kwamba kikao kile kilifanyika ndani ya “Al-Kaaba”, baada ya kipindi kirefu cha kuchangia fikra na mawazo ndipo wakakubaliana kwa kauli moja kuwa wamfanye kuwa ni hakimu mtu yeyote atakayekuwa wa mwanzo kuingia mle kupitia “Baniy Shaybah”, mlango huu leo unajulikana kama “Babus-Salaam”. Hivyo wote wakayakazia na kuyakodolea macho yao upande wa mlango ule, kwa hekima anazozijua mwenyewe Mwenyezi Mungu akajaalia wa mwanzo kuingia baada ya muafaka ule awe ni Bwana Mtume – Rehma na Amani zimshukie -. Alipoingia tu wote wakamfurahikia na kumpokea kwa shangwe huku wakisema “Huyu ni mtu mwaminifu na sote tunamkubali na kumridhia”. Wakamuhadithia tatizo lao nae aliwasikiliza kwa makini kabisa. Walipomaliza akaikunjua shuka yake ya kujitanda na kuitandika chini, kisha akalichukua “Hajar Aswad” na kuliweka katikati ya shuka ile, hapo ndipo alipomtaka kila kongozi wa kabila kuliwakilisha kabila lake kwa kunyanyua ncha ya shuka ile. Wakalibeba “Hajar Aswad” wote kwa pamoja mpaka mahala linapotakiwa liwekwe. Hapo sasa ndipo Bwana Mtume akalichukua kwa mkono wake mtukufu na kuliweka mahala pake. Kwa hekima yake hiyo, mzozo ule ukaisha na makurayshi wakashangazwa sana na upeo wa kufikiri na uelekevu wa akili ya Bwana Mtume, kijana mwenye umri usiopindukia miaka thalathini na tano akaweza kufanya walichoshindwa kukifanya watu wazima na akawa ameinusuru jamii yake na janga la balaa ya vita vya wenyewe kwa wenyewe lililokuwa linawojongolea kutokana na mzozo wa uwekaji “Hajar Aswad”.

ii) VITA VYA FUJJAAR NA VIAPO VYA NUSRA

Bwana Mtume – Rehma na Amani zimshukie – alijenga moyo wa kushirikiana na jamii yake katika kazi zote za ujenzi wa jamii yake kama tulivyoona namna alivoshiriki katika ujenzi wa Al-Kaaba. Kwa upande mwingine alikuwa akichukia sana kushirikiana nao katika zile ada na desturi mbaya japokuwa jamaa zake walitamani ashirikiane nao lakini mara zote alikuwa akiwakatalia. Vita vya “Fujjaar” ni ushahidi tosha uonyeshao jinsi Mtume Muhammad alivyoshirikiana na jamii yake. Alipofikia umri wa miaka kumi na tano au ishirini alijiunga na jamii yake katika vita vya Fujjaar. Sababu ya vita hivi ilikuwa ni kulinda na kuhifadhi heshima na utukufu wa ile miezi minne mitukufu iliyotajwa ndani ya Qurani ambamo vita vimeharamishwa. Mojawapo la makabila ya Hijazi ilivunja utukufu wa miezi ile kwa kulishambulia kabila jingine ndani ya miezi ile mitukufu, ndipo makabila mengine yakajiunga pamoja kuliadabisha kabila lile chokozi. Kazi ya Bwana Mtume katika vita hivi ilikuwa ni kuwakusanyia silaha wapiganaji na wakati mwingine ilimbidi kushiriki moja kwa moja katika medani ya vita. Vita hivi vilidumu kwa kipindi kisichopungua miaka minne, vikaisha kwa kuwekeana mkataba wa suluhu na amani baina ya zile pande mbili husika huku upande wa uliopoteza idadi kubwa ya watu ukilipwa fidia na upande mwingine.

Viapo vya Nusura : hili ni tukio lililotokea wakati Mtume Muhammad akiwa na umri wa miaka ishirini. Viapo vya nusra ilikuwa ni mojawapo ya maazimio ya kikundi cha kutetea haki ambacho kimsingi ilikuwa ni kumtetea mtu mnyonge asidhulumiwe, kumpatia haki kila mwenye kuistahiki na kumsaidia kila mwenye haja na matatizo. Maazimio ya kikundi hiki yalipitishwa ndani ya nyumba ya Bwana Abdillah bin Jad’aan Al-Tamiymi, huyu alikuwa miongoni mwa viongozi wa makurayshi . Mtume Muhammad aliona hii ndio fursa aliyoitamani na kuingojea kwa muda mrefu ili aweze kushirikiana na jamii yake katika kuyapiga vita maovu na dhuluma iliyoitawala jamii yake. Hivyo basi kutokana na azma hiyo alishiriki kikamilifu na ami zake katika kikao kile na kuwa miongoni mwa walioshiriki kuyapitisha maazimio yale matukufu.

 


TUJIFUNZE Tabia njema ndio siri kubwa ya mafanikio ya mtu. Mwenyezi Mungu amwambia Mtume wake : “BASI KWA SABABU YA REHEMA ITOKAYO KWA ALLAH UMEKUWA LAINI KWAO (Ewe Muhammad) NA KAMA UNGEKUWA MKALI NA MWENYE MGUMU BILA SHAKA WANGALIKUKIMBIA [3:159]

TUJIFUNZE : Kiongozi bora ni yule anayekubalika na watu wake, haya yanathibitishwa na makurayshi walipomwambia Mtume : “Huyu ni mtu mwaminifu na sote tunamkubali na kumridhia”.

TUJIFUNZE : Kiongozi mzuri ni yule anayechukia maovu yanayotendwa na jamii yake na kuyatafutia ufumbuzi muafaka. Mwenyezi Mungu anatuambia : “BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA (ruwaza nzuri) KWA MTUME WA ALLAH, KWA MWENYE KUMUOGOPA ALLAH NA SIKU YA MWISHO NA KUMTAJA ALLAH SANA” [33:21]


Forum | Guestbook | Tuandikie |