|
I.
Mauaji ya Abu Raafii:
Katika mwezi wa Ramadhani
(Desemba 627 A.D.), Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alimtuma Abdullah
Ibn Atiyk kwenda Khaybar pamoja na watu wanne wa kabila la Khazraj. Aliwatuma
kwenda kumuua mmoja wa viongozi wa Khaybar; Abu Raafii Salaam Ibn Abil-Haqiyq.
Huyu alikuwa ni mmojawapo wa viongozi wa Mayahudi Banin-Nadhwiyr waliohamia
Khaybar baada ya kufukuzwa Madinah na kuchukua uongozi wa hapo Khaybar.
Alikuwa ni mfanyabiashara maarufu tajiri anayemiliki biashara nyingi mpaka
akawa anaitwa “Tajiri wa Hijaazi”. Na alikuwa ni miongoni mwa waliochangia kwa
ari na mali kuyakusanya majeshi shirika dhidi ya Mtume wa Allah katika vita
vya Khandaq. Akawasaidia mushrikina katika vita hivi kwa kuwapa mali nyingi
mno, vita hivi vilipotamatia kwa kushindwa majeshi shirika na kuuawa kwa Baniy
Quraydhwah. Hakukubali kushindwa, akaenda kuwashawishi Ghatwfaani na
mushrikina wengine wa Kiarabu waliomzunguka kujiunga upande wake kwa pamoja
waunde jeshi kubwa litakalo weza kumsagasaga Mtume na maswahaba wake.
Ndipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akamtumia watu
watano hawa wa kabila la Khazraj kumuua mtu huyu mwenye dhamira mbaya
kuwaelekea waislamu na Mtume wao. Na akawakataza kuua mtoto au mwanamke,
wakatoka mpaka wakafika Khaybar, wakajificha mpaka zilipotulia harakati za
mchana kutwa. Ndipo wakamuendea muovu huyu nyumbani kwake usiku wakiongozwa na
Abdullah Ibn Abiy Atiyk kwa kuwa ndiye aliyekuwa akiongea Kiyahudi.
Walipofika, akabisha hodi na kusema: Nimemletea zawadi Abu Raafii, mkewe
akamfungulia mlango. Mwanamke yule alipoziona silaha akataka kupiga kelele,
wakamnyooshea mapanga akafunga domo lake. Wakaingia alipo kuwa mumewe; Abu
Raafii na kuanza kumshambulia kwa mapanga yao bila ya kumpa nafasi ya
kujitetea, Abdullah Ibn Unaysi akamrukia na kumshindilia panga la tumbo
likatokeza upande wa pili na kumuua. Walipokwishamuua wakateremka chini na
kuondoka zao, hapo ndipo mkewe alipoweza kupiga kelele za kuomba msaada na
kupokewa na watu wengine.
Abdullah Ibn Abiy Atiyk alikuwa na matatizo ya macho; haoni
vizuri, akaanguka ngazini walipokuwa wakishuka. Akaumia vibaya mguu wake,
wenzake wakambeba na kwenda nae mpaka katika dampo (mahala pa kutupia taka) la
mji, wakajificha hapo. Huku nyuma watu wakatoka kuitika kelele zile za msaada
na kuanza kuwatafuta wakiwa na vijinga vya moto, lakini hawakufanikiwa
kuwaona. Wakaendelea kujificha mahala hapo mpaka zilipotulia harakati za
kuwasaka. Wenyewe wanasimulia: Tukambeba mwenzetu na kufika kwa Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-tukampasha khabari ya kuuawa kwa adui wa Allah
huku kila mmoja wetu akidai kumuua yeye. Mtume akasema: “Hebu leteni panga
zenu”, kila mmoja akawa anampa panga lake akiliangalia, akasema alipolishika
panga la Abdullah Ibn Unaysi: “Huu ndio upanga uliomuua, ninauona una athari
ya chakula”.
II.
Kujilinda dhidi ya hujuma:
Hivi ndivyo
ulivyomalizika mwaka huu wa sita tangu kuhamia Madinah kwa mapambano mepesi
mepesi kama haya. Mapambano yaliyoendeshwa kwa njia ya kumshtukiza na
kummaliza adui kabla hajaanza kushambulia. Na lengo la mashambulizi haya
halikuwa ni kuanza uchokozi na uadui, kwa sababu kuanza uchokozi na uadui ni
msingi na sera isiyokubaliwa na Uislamu. Hakika si vinginevyo, lengo lilikuwa
ni kujilinda dhidi ya hujuma tarajiwa iliyothibiti na wala si vinginevyo.
Allah Taala anawaambia waislamu: “NA PIGANENI KATIKA NJIA YA ALLAH NA WALE
WANAOKUPIGENI, WALA MSIPINDUKIE MIPAKA (mkawapiga wasiokupigeni). KWANI ALLAH
HAWAPENDI WARUKAO MIPAKA”. [2:190]
Kwa hivyo basi, mapambano haya mepesi mepesi yaliyotokea,
hakika si vinginevyo yalikuwa ni kwa ajili ya kujibu na kuurudi uadui na
uchokozi aliouanza adui. Au yalikuwa na nia ya kumkho fisha adui aliyekuwa na
dhamira ya kufanya uchokozi. Na bila shaka mapambano na mashambulizi haya
yalifanikiwa kufikia malengo yake kwa kiasi kikubwa kabisa. Kwani mwaka wa
sita haukumalizika ila na haiba ya waislamu ikawa imeshaziingia nafsi za
makabila ya Kiarabu yaliyokuwa majirani na Madinah. Na hali ya hewa ikaanza
kuwa ya utulivu na amani baina ya waislamu na majirani zao. Na ikawa
inamkinika kuanzisha mafungamano na mahusiano ya ujirani mwema baina yao kwa
kuyapisha yapite yaliyokwishapita na kuzizika tofauti zao. Na kuanzisha
ukurasa mpya wa ushirikiano chini ya anga la amani na utulivu.
|