|
Ilikuwa ni fursa na
wakati muafaka wa kuizuru nyumba ya Allah (Al-Ka’abah), Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie-akaazimia kufanya ziara hiyo pamoja na wafanya ziara
wengine miongoni mwa Waarabu. Ni katika mwaka huu wa sita pia, ndimo
ilimofaradhishwa nguzo ya tano ya Uislamu; ibada ya Hijjah sambamba na ile ya
Umrah. Usiku mmoja Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliona ndotoni
kwamba yeye na maswahaba wake wanaingia katika nyumba tukufu ya Allah. Wakiwa
ni wenye amani, wamenyoa nywele na wengine kupunguza wakiwa hawamkhofu adui
atakayewazuia wasiingie. Mtume akafurahishwa sana na ndoto yake hii na
akawasimulia maswahaba wake, nao pia wakafurahi na kujawa na furaha.
Wakaiyakinisha ndoto hiyo ya Mtume kuwa ni ukweli utakaotokea bila ya shaka,
kwa sababu waliamini kuwa ndoto za mitume huwa ni kweli na haki. Ndoto hizo
huwa ni ilhamu kutoka kwa Allah juu ya jambo litakalotokea kabla ya kudhihiri
kwake katika ulimwengu wa maono. Kwa hivyo shauku ya Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-na ile ya waumini katika kuizuru Al-Ka’abah ikarudufishwa na
kuamshwa na ndoto hii. Ndipo Mtume alipotia azma ya kuizuru nyumba hii tukufu
ya Allah katika mwaka huu. Fursa na mazingira yalikuwa muafaka yanayoruhusu
kufanyika kwa ziara hii, kwani tayari amani imekwisharejea tena Madinah baada
ya kutimuliwa kwa Mayahudi. Wanafiki wamevunjwa nguvu baada ya kuondoka kwa
washirika na wafadhili wao wakuu na mabedui huko majangwani wamekuwa si
tishio tena kwa waislamu bali waislamu ndio wamekuwa tishio kwao. Wote hawa
walitishwa na nguvu ya waislamu katika kuitetea, kuilinda na kuihami imani
yao, kwa hivyo kitisho cha Uislamu kikazitamalaki nyoyo zao na kuzitetemesha
nafsi zao. Msimu wa ibada ukawadia na Waarabu kutoka pande za mbali na zile za
karibu wakaanza kujiandaa kwa ajili ya ziara hii tukufu. Kwa nini basi
waislamu wasiitumie fursa hii, wakaikusudia nyuma tukufu pamoja na wakusudiaji
wengine na wakaingia pamoja na wenye kuingia?! Laala (pengine) Makureishi
zimelainika tabia zao na kupunguza uadui wao dhidi ya Uislamu na waislamu
baada ya kushindwa kwa njia zote za nguvu walizojaribu kuzitumia. Kila
walipojaribu kuudhoofisha Uislamu ndio ulikuwa ukizidi nguvu na kila jaribio
la kuuzima ndio lilizidisha nuru yake. Kila walipofanya jaribio la kuutokomeza
ndio watu walizidi kuujongelea na kuingia makundi kwa makundi. Kwa
kuyazingatia yote haya haikupita katika dhana kwamba Makureishi watawazuilia
waislamu peke yao kufanya ziara ya nyumba hii. Nyumba iliyofanywa sawa sawa
kwa watu wote, kwa wakaao humo na wale wageni.
Ikiwa watawazuia watakuwa
wameudhihirishia ulimwengu udhalimu na uadui wao. Ili Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-awakatie Makureishi hoja zote na kuwahakikishia wao na watu
wote. Kwamba yeye hakika si vinginevyo amekuja katika nyumba ya Allah kufanya
ziara kwa amani na kwamba hakuja kwa vita. Ibn Is-haaq-Allah
amrehemu-anahadithia: “Alitoka katika mwezi wa Dhul-Qa’adah kwa ajili ya
kufanya Umrah akiwa hataki vita. Akawatolea wito wa kutoka pamoja nae majirani
zake miongoni mwa watu wa vitongoji vilivyoizunguka Madinah. Alifanya hivyo
huku akichelea Makureishi wasije kumtangazia vita au kumzuia kuingia Makah”.
Lakini Mabedui (wakazi wa vitongojini) aliowataka kutoka pamoja nae,
walidhania kwamba lazima tu vitazuka vita baina ya Mtume na Makureishi. Na
kwamba Mtume na maswahaba wake watahiliki tu katika vita hivi, kwa ajili hii
wakakataa kuambatana na Mtume katika safari hii ya hatari, wakichelea kujitia
maangamivuni wao wenyewe. Ibn Is-haaq-Allah amrehemu-anaendelea kuhadithia:
“Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akatoka na Muhajirina na Answari na
baadhi ya Waarabu waliojiunga pamoja nao. Akawaswaga pamoja nao wanyama wa
sadaka; ngamia sabini na akahirimia Umrah ili kuwatoa watu wasiwasi wa vita.
Na ili watambue kwamba yeye hakika si vinginevyo ametoka kwa ajili ya ziara ya
nyumba tukufu ya Allah na kuiadhimisha”.
IV.
Mtume atoka na maswahaba
wake bila ya silaha:
Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akamuachia ukhalifa wa Madinah, Abdullah
Ibn Ummu Maktuum, swahaba wake aliyekuwa kipofu. Katika safari yake hii
akaambatana na mkewe Ummu Salamah, akatoka Madinah mwezi mwandamo wa
Dhul-Qa’adah (Februari 628 A.D.). Akatoka akiwa na waislamu wapatao alfu moja
na mia tano wakiwa hawakuchukua silaha zaidi ya majambia yao yaliyofutikwa
kwenye ala zake. Hizi zilikuwa ni silaha za kawaida ambazo kila msafiri hana
budi kuchukua katika Bara Arabu wakati huo. Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akampanda ngamia wake aliyekuwa akiitwa “Al-Qaswaa”, akaenda na
maswahaba wake mpaka wakafika “Dhul-Hulayfah’. Hapa ni mahala palipokuwa kiasi
cha umbali wa maili sita kutoka Madinah, wakaswali Adhuhuri hapo. Baada ya
kumaliza kuswali akaamuru waletwe ngamia, wakavishwa vitambaa, wakatiwa alama
zioneshazo kuwa ni wanyama wa sadaka na kuvikwa shingoni mwao kitu mithili ya
vidani. Hii ndio ilikuwa ada na desturi ya Waarabu kwa wanyama wanao wachukua
kuwachinja na kuwatoa sadaka katika msimu wa Hijjah. Kisha ndipo akahirimia
Umrah na kufuatiwa na maswahaba, halafu ndipo msafara wa kuelekea Makkah
ulipoanza. Wakiwa wamevaa mavazi ya Ihraamu wakileta Talbiyah: “LABBAYKA
ALLAAHUMMA LABBAYKA, LABBAYKA LAA SHARIYKA LAKA LABBAYKA, INNAL–HAMDAH
WAN-NI’IMATA LAKA WAL-MULKU, LAA SHARIYKA LAKA”. Maana: “Labeika (nakuitika)
ewe Mola wa haki labeika, labeika huna mshirika labeika. Hakika himda njema,
neema (zote) na ufalme ni wako, huna mshirika”. Ikawa kila anayewaona katika
mandhari hii nzuri ya kupendeza, hana shaka kwamba wao wanakuja kwa amani,
hawakusudii ila kutekeleza ibada zao tu basi. Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akamtanguliza mbele yao Ubbaad Ibn Bishri pamoja na wapanda wanyama
ishirini. Ili wawe watangulizi wao wa kuangalia usalama wa njia na akamtuma
Bishri Ibn Sufyaan kama mpelelezi wake kwa Makureishi. Akapeleleze dhamira na
maoni yao juu ya ziara yake hii aliyoikusudia na kisha aje kumpasha khabari
kabla ya kuingia Makkah.
|