|
Makureishi walipandwa na mori/hamasa za kijahilia
pale zilipogonga ngoma za masikio yao khabari za ujio wa Mtume wa Allah.
Wakashika msimamo wa kutokumruhusu Mtume kuingia Makah kwa namna yo yote iwayo
na wakaanza kujiandaa kwa vita ikiwa atang’ang’ania kuingia bila ya ridhaa
yao. Wakamtuma Khaled Ibn Al-Waleed na Ikrimah Ibn Abu Jahli kuliongoza kundi
la mashujaa wao mia mbili, kwenda “Kuraail-Ghamiym” kuwazuia waislamu
wasiingie Makah. Wakawatolea wito wa kutoka pamoja nao washirika wao katika
Wahabeshi na watu wa Thaqiyf. Wakatoka wakaenda mpaka wakafika mahala paitwapo
“Baldahi”, nje kidogo ya Makah wakapiga kambi hapo. Wakasimika mahema na
kujenga vibanda vya muda, wakakaa na wake na watoto wao na wakaweka wapelelezi
juu ya majabali kuchunguza harakati zote za adui yao. Kisha wapelelezi hawa
wakawa wakipashana khabari kwa sauti, wakisema: “Muhammad amefanya kadha wa
kadha”, wakipokezana hivyo mpaka khabari zikifika kambini kwao.
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipofika mahala
panapoitwa “Usfaani” na akawa umbali wa mwendo wa siku mbili kutokea Madinah.
Akakutana na Bishri Ibn Sufyaan, huyu akampasha khabari za Makureishi, Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipozisikia khabari hizi akasema: “Ee ole
wao Makureishi, wameshaliwa na vita! Wangelipatwa na nini lau kama
wangeliniachia njia pamoja na watu wengine. Ikiwa watanigusa, kitakuwa hicho
wakitakacho na iwapo Allah atanipa ushindi wataingia Uislamuni kwa makundi?
Wallah, sitaacha kuendelea kupigana nao kwa ajili ya hiki alichonituma kwacho
Allah, mpaka Allah aipe ushindi dini hii au mimi nife!”
SOMO LA TANO.
I.
Mtume ajitahidi kwa
jitihada zote kuepusha vita:
Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-hakupendelea kabisa kuzuka kwa vita na alijitahidi sana
kuonesha kuwa safari yake hii ni safari yenye malengo ya amani. Safari
iliyojitenga na sababu zote zinazoweza kuitia dosari na imeepukana na mambo
yote yanayo pingana na malengo yake. Pamoja na jitihada zote hizi za makusudi
katika kuepusha vita, alipoona Makureishi wamejiandaa kwa vita na wametuma
vikosi tangulizi ili kumzuia asiingie Makah. Na wanatumia nguvu kumzuia
kufikia lengo la safari yake hii ambalo si jingine zaidi ya kuizuru nyumba
tukufu ya Allah. Akaonelea ni vema abadili muelekeo na njia ya safari yake,
badala ya kupita njia ambayo tayari ina kizuizi cha Makureishi walio tayari
kwa vita, apite njia nyingine ili kuepusha vita. Kwani kama atashikilia tu
kupita njia hiyo hiyo ya kawaida ni lazima tu atakutana na Makureishi. Ambao
huenda watamlazimisha kuingia katika matumizi ya nguvu ambayo hakuyapendelea,
hapo ndipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipowaambia maswahaba
wake: “Nani atakayeweza kutupitisha njia nyingine isiyo hii?”. Akaja mtu mmoja
kutoka katika kabila la Aslama, akawaongoza katika njia ngumu sana iliyowawia
uzito waislamu kuipita. Kisha akawapitisha katika ardhi tambarare kwenye bonde
la ufa, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaamuru wapite upande wa
kulia. Wakaenda mpaka wakafika kwenye maporomoko ya Hudeibiyah kwa chini ya
Makah umbali wa mwendo wa siku moja mpaka kuingia Makah.
Walipofika mahala hapo, ghafla ngamia wa Mtume aliyekuwa
akiitwa “Al-Qaswaa” akakita magoti na kugoma kuendelea na safari. Watu
wakaanza kumpigia kelele ili ainuke na kuendelea na safari, makelele yao hayo
hayakusaidia kitu kwani Al-Qaswaa hakuinuka. Watu wakashangazwa mno na tukio
hili, wakasema: “Al-Qaswaa amegoma kufuata amri (ameasi)”. Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akawajibu: “Hajagoma na wala hana tabia hiyo,
lakini kilichomzuia kusonga mbele ni kile kile kilichowazuia watu wa ndovu
kuingia Makah. Namuapia yule ambaye nafsi ya Muhammad i mkononi mwake, leo
Makureishi hawataniitia hatua ambazo wataniomba ndani yake kuunga udugu na
kuyaadhimisha matukufu ya Allah, ila nitawaitika”. Halafu akawaamuru watu
kupiga kambi hapo hapo walipo. Na mahala hapo palikuwa ni bonde kame lisilo na
maji zaidi ya maji kiduchu tu yaliyokuwa katika shimo moja tu. Watu wakaanza
kuyatumia maji yale kidogo kidogo na kwa uangalifu mkubwa mpaka yakaisha.
Walipoyamaliza na pakawa hapana tena tone la maji, wakamshtakia Mtume wa Allah
kiu chao. Nae Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akaja akakaa kwenye ukingo wa
kisima (shimo) kile, akaomba aletewe ndoo yenye maji ya kisima hicho.
Akaletewa, akachota choto moja akasukutua na kuomba Mungu, kisha akayatemea
kisimani mle na kuwaambia: “Kiacheni kisima hiki kwa muda”, wakakiacha kwa
kitambo kidogo tu, basi haukupita muda ila maji yake yalijaa na kufurika. Watu
wakanywa, wakanywa hata kikakatika kiu na wakajitwaharisha na kuwanywesha
wanyama wao. Wakaendelea kuyatumia maji yale bila ya kwisha mpaka wakaondoka.
II.
Mtume atangaza nia yake
ya amani kwa wajumbe wa Makureishi:
Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-alipotuama hapo Hudeibiyah, alijiwa na Budeil Ibn Warqaa
pamoja na kundi la watu wa kabila la Khuzaa. Wamekuja kumuuuliza madhumuni ya
msafara wake huu na ikumbukwe kwamba hawa Khuzaa walikuwa ni washirika wa
Mtume tangu zamani. Budeil alipofika kwa Mtume alimpasha khabari za maazimio
ya Makureishi na akamuuliza Mtume sababu/nia ya majaji yake haya. Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akamjibu: “Hakika sisi hatukuja kupigana na
mtu, sisi tumekuja kufanya Umrah tu. Ikiwa Makureishi watataka tutawapa muda
na watuachie njia tuingie Makah pamoja na watu wengine. Na iwapo watakataa,
basi naapa kwa yule ambaye nafsi ya Muhammad i mkononi mwake, wallah
nitapambana nao hadi kufa”. Budeil na ujumbe wake wakarejea kwa Makureishi na
kuwaambia: “Hakika nyinyi mnamfanyia haraka Muhammad, kwani yeye hakujia vita,
hakika si vinginevyo amekuja kuizuru Al-Ka’abah”. Wakasema: “Hata kama hakuja
kwa vita, basi wallah kamwe hataingia Makah kwa nguvu bila sisi kupenda wala
Waarabu hawatatuzungumza kwa unyonge huo katu”.
|