Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

I) MTUME AFANYA IBADA KATIKA PANGO LA HIRAA

Faida

Mtume wa Mwenyezi Mungu – Rehema na Amani zimshukie – alipokaribia umri wa miaka arobaini alipenda kukaa peke yake faraghani na kujitenga na jamii yake; jamii ya watu wa Makkah. Jamii iliyozama katika kiza cha ushirikina na tabia mbaya zisizo na chembe ya utu. Kujitenga huku hakukuwa ni kwa sababu alikuwa anaichukia jamii yake, la hasha. Bali ni kwa ajili ya kuyachukia maovu yaliyokuwa yakitendwa na jamii yake. Kwa hivyo akaonelea ni vema akae faraghani atafakari ni jinsi gani atakavyoweza kuinusuru na kuitoa jamii yake katika itikadi ile potofu ya ushirikina, itikadi ya kuyaabudia masanamu yaliyotengenezwa na mikono yao wenyewe.

Baada ya kufikiri kwa kina, ni wapi katika mji wa Makkah ambapo anaweza kupata nafasi ya faragha, hakupapata. Hapo ndipo akaamua atoke nje kabisa ya mji wa Makkah. Akaamua ajitenge kwa kukaa ndani ya pango la “Hiraa”. “Hiraa” ni pango dogo lililopo juu ya jabali Nuur. Jabali hili liko kiasi cha umbali wa wa maili tatu kutoka mji wa Makkah, mahala pasipo na nyumba wala mashamba. Pango la “Hiraa” lilikuwa linatisha na lenye upweke mkubwa, upweke ambao ulizidishwa na kiza kilichotanda mahala pale. Hapa ndipo Mtume aliona patamfaa kutafakari jinsi ya kuikomboa jamii yake kutokana na utumwa wa ushirikina. Akawa anachukua chakula cha kutosha kutoka kwa mkewe Bi Khadija na kwenda zake faraghani katika pango la Hiraa. Huko alikaa kiasi cha siku kumi na mara nyingi akitimiza mwezi kamili. Kazi kubwa aliyokuwa akiifanya huko ilikuwa ni kumuabudu Mola wa haki kupitia mafundisho sahihi yaliyoachwa na babu yake, Nabii Ibrahim – Rehema na Amani ziwashukie wote -. Athari ya mafundisho ya Nabii Ibrahim alikuwa ingali hai miongoni mwa makurayshi wachache ambao waliendelea kufanya ibada kwa mujibu wa mafundisho hayo. Naye Mtume akawa anafanya ibada kwa kuufuata muongozo huo huo.

 SURA YA PILI

SOMO LA KWANZA

i) KUPEWA UTUME

Mtume Muhammad – Rehema na Amani zimshukie – alipofikia umri wa ukamilifu, umri ambao akili ya mwanadamu huwa imepevuka na kukomaa, umri wa miaka arobaini. Huu ukawa ndio wakati muafaka wa kupewa kazi nzito, ngumu na yenye kuhitaji subira ya kutosha. Kazi ya kuinusuru jamii yake na kiza totoro cha ushirikina. Hapo ndipo Mwenyezi Mungu Mtukufu akamkabidhi dhamana ya utume, awabashirie watu wema kupata pepo ya milele kwa kumfuata na awakhofishe na adhabu kali ya moto wa milele wale wote watakaomkadhibisha na kuacha kumfuata. Awalinganie watu kuwatoa katika viza vya ushirikina kuwapelekea katika nuru ya kumpwekesha Mwenyezi Mungu asiye na mshirika.

Katika usiku wa mwezi kumi na saba (17) Ramadhan mwaka wa kumi na tatu kabla ya hijra sawa na Mwezi Julai mwaka mia sita na kumi na moja (611) Miladia Mtume akiabudu faraghani ndani ya pango la Hiraa hapo ndipo ulipomshukia wahyi/ufunuo kwa mara ya kwanza. Jibriil –Amani imshukie – malaika mwaminifu wa wahyi alimtokezea na kumwambia “Soma” Mtume akamjibu “Mimi si mwenye kusoma” Jibril akamshika Mtume na kumgandamizia kifuani kwake kama vile anamkaba, kisha akamuachia na kumwambia tena “Soma” Mtume akamjibu kama alivomjibu mwanzo “Mimi si mwenye kusoma” Jibril akamkamata tena na kumgandamiza na kumwambia “Soma” hii ikiwa ni mara ya tatu, Mtume akauliza “Nisome nini ?” Hapo sasa Jibril ndipo akamwambia : SOMA KWA JINA LA MOLA WAKO ALIYEUMBA, AMEUMBA MWANADAMU KWA PANDE LA DAMU. SOMA NA MOLA WAKO NI KARIMU SANA. AMBAYE AMEMFUNDISHA (Binadamu elimu zote hizi) KWA WASITA (msaada) WA KALAMU (zilizoandika vitabu, watu wakapata elimu) AMEMFUNDISHA MWANADAMU (chungu ya) MAMBO ALIYOKUWA HAYAJUI” [96:1-5]

Kisha Jibriil akashika njia akaenda zake, naye Mtume kwa wepesi akarejea kwa mkewe Bi Khadija akiwa amejawa na khofu kubwa kutokana na kiumbe mgeni, malaika kwa mara ya kwanza. Akasema “Nifunikeni ! Nifunikeni!” Mkewe akamfunika maguo kutokana na alivyokuwa akitetemeka kama mtu mwenye homa kali kabisa. Alipotulizana ndipo akamuuliza kulikoni, mbona yuko katika hali hiyo? Mtume akamuhadithia mkewe hali ilivyokuwa mwanzo hadi mwisho na kusema “Ninaichelea nafsi yangu na shetani/pepo mbaya” mkewe akamtuliza na kumwambia “Sivyo hivyo ! Wallah Mwenyezi Mungu kamwe hatokufedhehesha. Kwani unaunga udugu, unasema kweli, unasaidia mnyoge, unamkirimu mgeni, unawapa sadaka masikini na unasaidia katika majanga”

Halafu ndipo Bi Khadijah alipoamua kumpeleka Mtume kwa mwana wa ammi yake Waraqah ibn Naufal, huyu alikuwa ni mwanachuoni mwenye elimu ya vitabu vitakatifu kabla ya Qur-ani {Taurati, Zaburi na Injili}. Bi Khadijah akamuhadithia binamu yake yote yaliyomtokea Mtume kama alivomueleza mwenyewe. Waraqah kutokana na elimu aliyokuwa nayo akamtoa wasiwasi Mtume na kumwambia “Huyu ndiye Naamus {Jibril} aliyekuwa akimshukia Issa bin Maryam, basi furahi kwani wewe ndiye Mtume wa umati huu”

Baada ya hapo wahyi ulikatika kwa kipindi kirefu, kukawa hakuna mawasiliano yoyote baina ya mbinguni na ardhini. Kukatika huku kwa wahyi hakukuja kwa bahati mbaya tu, bali hekima yake ilikuwa ni kuizidisha shauku na kiu ya Mtume kwa wahyi. Mtume akapatwa na huzuni kuu na akawa akienda na kurudi pangoni Hiraa, huenda pengine Jibril atamjia tena, lakini wapi hakumuona. Hali ilikuwa hivyo mpaka Mtume akadhania kuwa Mola wake amemkasirikia na kumtupa. Baada ya kipindi hicho kigumu ndipo Wahyi ulipoanza kushuka tena na Mola wake akamtuliza kwa kumwambia : “HAKUKUACHA MOLA WAKO WALA HAKUKASIRIKA (nawe Ewe Nabii Muhammad) NA BILA SHAKA (kila) WAKATI UJAO (utakuwa) NI BORA KWAKO KULIKO WAKATI ULIOTAGULIA” [93:3-4]

Kisha tena ikamshukia kauli yake Mola : “EWE ULIYEJIFUNIKA MAGUO. SIMAMA UONYE (viumbe) [74:1-2].

Huu ndio ukawa ndio mwanzo wa kazi na safari ndefu yenye taabu na misukosuko mikubwa ya kufikisha ujumbe wa Mola wake Mtukufu kwa watu wote.

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI : kuwa kiongozi ni mtumishi wa watu wake kwani uongozi ni majukumu na utumishi na sio utukufu na utumikiwa. Ni kutokana na uzito, dhamana na majukumu ya uongozi ndipo Bwana Mtume akatuhadharisha kwa kusema “HAKUNA KHERI KATIKA UONGOZI KWA MTU MUISLAMU” Ahmad. 

 TUJIFUNZE NA TUKUBALI : Kuwa Uislamu ni ELIMU na hili linathibitishwa na historia ya Uislamu wenyewe. Amri ya kwanza kutoka mbinguni ilikuwa ni amri ya kusoma, kwa kuwa elimu ndio msingi wa kila kitu. Ili kuusisitiza umuhimu wa elimu ndipo Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – akatuambia “Kutafuta elimu ni faradhi ya kila mwislamu” Al-Baihaqiy. Haya shime na tusome, ewe ndugu yangu muislamu.


Forum | Guestbook | Tuandikie |