|
Akainuka Urwah Ibn Masoud; kiongozi wa kabila la
Thaqiyf, huyu alikuwa ni mtu mwenye sauti na busara, akawaambia: “Bila ya
shaka mtu huyu (Muhammad) amekupeni mipango ya uongofu, basi ikubalini, hebu
niacheni nikazungumze nae”. Wakamwambia: “Nenda”, akamuendea Mtume na
kumwambia: “Ewe Muhammad, hakika mimi nimewaacha huko watu (jamaa) wako
wamewatolea wito watu kutoka kuja kupambana nawe. Nao wameapa kwa Allah kwamba
hawatakuruhusu kuifikia Al-Ka’abah ila uwaue wote. Hakika si vinginevyo, mbele
yako una mambo mawili tu ya kuchagua; ama uwasagesage na kuwaua watu wako
upate kuifikia Al-Ka’abah, nasi hatujapatapo kumsikia mtu aliyewamaliza watu
wake kabla yako. Au wakutupe na kukuacha peke yako hawa watu ulio nao, kwani
mimi naona watu ulio nao ni watu hovyo hovyo tu wasio na muelekeo wala
hazijulikani nasabu zao”. Sayyidina Abu Bakri-Allah amuwiye radhi-akamshtumu
na kumwambia maneno makali: “Ole wako wee! Hivi sisi tunaweza kumtupa mkono na
kumuacha peke yake?”
Wakati Urwah alipokuwa akiongea na Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-alikuwa akizishikashika ndevu za Mtume. Alifanya hivyo ikiwa
ni kufuata ada/desturi ya Waarabu wakati wanapokuwa na mazungumzo yenye nia ya
kuunga udugu na kuleta mapatano. Wakati akifanya ada hiyo, Mugheerah Ibn
Shu’ubah ambaye ni mwana wa kaka yake Urwah, alikuwa amesimama karibu kabisa
na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Akiwa amevaa kofia ya chuma na
kushika upanga, kila mara Urwah alipokuwa akiunyoosha mkono wake kuzishika
ndevu za Mtume, Mugheerah aliugonga mkono wake kwa ubapa wa upanga huku
akimwambia: “Ondosha mkono wako usoni kwa Mtume wa Allah kabla sijaukata”.
Urwah nae akamjibu akiwa hamjui (kuwa ni mwana wa nduguye): “Ole wako! Ukali
na ugumu wa moyo ulioje uliokuvaa!”, Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akitabasamu (kutokana na majibizano hayo baina ya mwana na ami
yake).
Urwah akaondoka kwa
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akiwa ameguswa mno na jinsi maswahaba
wanavyo mpenda na kumuadhimisha Mtume wao. Na namna wanavyo shindana kumtii na
kutekeleza amri yake, akarejea kwa Makureishi na kuwaambia: “Enyi kusanyiko la
Makureishi! Hakika mimi nilimtembelea Kisra katika ufalme wake, nikamtembelea
Qayswar katika ufalme wake na Najaashi katika ufalme wake. Hakika wallah, mimi
sijapatapo kumuona mfalme kwa watu wake kama alivyo Muhammad kwa maswahaba
wake! Wallah, hawamkazii macho, hawainui sauti zao mbele yake na kunamtoshea
yeye kuashiria tu jambo na likatendwa. Na nimewajaribu watu hao (waislamu),
nikagundua ni watu wasiojali kitawapata nini katika kumlinda mtu wao (Mtume),
haya basi ifikirieni upya rai yenu. Yeye amekwisha kuelezeni mipango yake,
basi enyi watu nyie wekeni muda wa amani baina yake nanyi na muukubali mpango
aliokuja nao kwenu. Hakika mimi ni mtoa ushauri nasaha kwenu pamoja na
kuchelea kwangu kuwa huenda msiushike na kuufuata!”. Makureishi
hawakuisikiliza rai na ushauri mzuri wa Urwah na wala hawakuiitika suluhu
aliyo waraghibishia. Urwah hakuwa na la kufanya kwa vichwa maji hawa ila
kurejea Twayf na kundi (ujumbe) lake.
IV.
Ujumbe wa Hulaysi;
kiongozi wa Wahabeshi.
Hulaysi Ibn Alqamah;
kiongozi wa Wahabeshi akasema: “Hebu niacheni nami nimuendee”, wakamwambia:
“Haya muendee”. Hulaysi alipochomoza kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-(Mtume) akasema: “Huyo ni fulani, nae ni katika watu wanaowatukuza
wanyama wa sadaka (hadyu), basi wawekeni wanyama hao mbele yake”. Wakafanya
kama alivyoagiza Mtume na wakampokea kwa mripuko wa Talbiyah. Hulaysi
alipowaona wanyama wa sadaka wakimiminika bondeni wakiwa wamepambwa na
akawaona waislamu wakiwa wamehirimia. Wakiwa wamechoka na nywele timtim
kutokana na uchovu wa safari ndefu. Hulaysi akaamua kurejea bila ya kufika kwa
Mtume kwa ajili ya kutukuza aliyoyaona na akawaambia Makureishi: “Wallah sisi
hatukufanya ushirika nanyi ili mumzuilie na nyumba ya Allah mtu aliyeijia
akiutukuza utukufu wake na kuitekeleza haki yake. Namuapia yule ambaye nafsi
yangu imo mikononi mwake, mumuachie ayatekeleze aliyoyajia au nitawatolea
wito Wahabeshi waondoke wote (na kukuacheni peke yenu)!”. Makureishi
wakamwambia: “Ewe Hulaysi wee! Yote uliyoyaona ni vitimbi na hila za Muhammad
na maswahaba wake, hebu tuache tukate shauri tutakaloliridhia sisi wenyewe”.
V.
Ujumbe wa Mtume kwa
Makureishi:
Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-akaona ni vema sasa yeye apeleke ujumbe wake rasmi kwa
Makureishi. Ili awathibitishie kwamba ni hakika yeye amekuja kuizuru nyumba ya
Allah na wala hakujia vita. Akamtuma Kharaash Ibn Umayyah Al-Khuzaaiy
kuwafikishia ujumbe wake huo, lakini wapi Makureishi wakaendelea kutia pamba
za masikio. Isitoshe wakamchinja ngamia wa mjumbe aliyetumwa kwao na Mtume na
tena wakataka kufika mbali zaidi kwa kumuua na mjumbe mwenyewe kama si
kuzuiliwa kufanya hivyo na Hulaysi; kiongozi wa Wahabeshi. Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akalistahamilia hilo na kuliona si kitu,
ijapokuwa kuwadhalilisha wajumbe ni jambo lisilostahamilika wala kusamehewa
miongoni mwa Waarabu. Ndipo tena Mtume alipoazimia kuwapelekea mtu wa karibu
mno nao, akamtuma Sayyidina Uthman Ibn Affaan. Mjumbe huyu wa pili wa Mtume wa
Allah, hakuweza kuingia Makkah mpaka alipochukuliwa dhamana na Abaana Ibn
Sa’ad Ibn Al-Aaswiy ambaye alikuwa ni binamu yake. Uthman akakutana na
viongozi wa Makureishi na kuwafikishia ujumbe wa Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie. Akawahakikishia ukweli wa nia ya majaji ya Mtume kuwa ni
kutaka kuizuru nyumba ya Allah. Lakini wapi bado Makureishi wakaendelea kuwa
ni viziwi wasiotaka kuisikiliza sauti ya haki wala kuitikia wito wa amani.
Uthmaan akajaribu kuwakinahisha kadri alivyoweza, lakini hawakukinahika na
badala yake wakaamua kumzuilia na kumshikilia kwa siku tatu. Kambini kwa
waislamu ikatangaa khabari kwamba Uthman ameuliwa, uvumi huu ukasambaa mpaka
ukamfikia Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kama kwamba ni kweli na
hakika isiyo na shaka.
|