|
I.
Kiapo cha utii (baia) cha
Ridhwaan.
Hapa
ndipo hali ya hewa ilipobadilika na kuwa si shwari tena na ikawa hapana budi
sasa tatizo hili lipatiwe ufumbuzi mwingine baada ya juhudi za kidiplomasia
kushindwa. Kwani tayari Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa
amekwisha itangaza wazi nia yake ya amani. Na akalidhihirisha hilo kwa kauli
sambamba na matendo yake tangu alipopiga hatua ya kwanza akitoka Madinah
kuelekea Makah. Na akawaitia Makureishi kwenye njia zisizo na matumizi ya
nguvu ili kuzuia umwagikaji wa damu usio wa lazima. Na ili kubakisha
mafungamano ya kidugu na kuhifadhi utukufu wa nyumba tukufu ya Allah na
kuchunga heshima ya mwezi mtukufu. Lakini wapi, njia zote hizi hazikusaidia
kuwalainisha Makureishi na kuwafanya wabadili msimamo wao shupavu. Mpaka
subira ikafikilia ukomo wake, hali ya hewa sasa ikawa haihitaji subira tena na
wala haiwezi kutengenea kwa subira aslani. Ikawa sasa matumizi ya nguvu
yakabiliwe na matumizi ya nguvu mfano wake, hapo ndipo Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-aliposema: “Hatutaendelea tena na hali hii ila kupambana na watu
hawa”. Na akawatolea waislamu wito wa kumbai (kula kiapo cha utii) juu ya vita
dhidi ya Makureishi. Watu wakaanza kuharakia kumbai huku wakipigana vikumbo na
kukanyaga vifaa/mizigo yao. Zoezi hili la baia lilipomalizika, wakachukua
silaha zao na kuwa tayari kwa vita. Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akambaia Uthman, akasema: “Hakika Uthman amekwenda kuitekeleza haja
ya Allah na haja ya Mtume wake, basi mimi ninafanya baia kwa niaba yake”.
Akakipiga kiganja chake cha kushoto kwa kile cha kulia na kusema: “Huu ni
mkono wa Uthman”.
Tukumbuke kwamba
maswahaba-Allah awawiye radhi-hawakuwa wamechukua silaha zaidi ya majambia
yao. Na wala hakukuwa na mizania ya idadi yao na ile ya Makureishi hata
kidogo. Pia hawakuwa na mavazi ya vita yatakayo wakinga na mapigo ya adui
katika medani ya vita. Na walikuwa wanajua kwa yakini kwamba kuingia vitani
katika mazingira hayo ni kuyahatarisha maisha yao. Lakini pamoja na yote hayo,
bado walimbai Mtume juu ya kuingia vitani kwa hamasa, ari, mori na nguvu
kubwa. Wakaziuza nafsi zao kwa Allah kwa ajili tu ya kupata radhi zake-Allah
awawiye radhi na awatakabalie baia yao hiyo takatifu. Baia yao hiyo ikawa ndio
sababu ya ushindi dhahiri wa kishindo ambao kwao Allah aliwafungulia waja wake
milango ya nusra na kheri. Na baada yake Uislamu ukawa katika mkondo wa
ushindi na nguvu mpaka ukazishinda dola zote zilizouzunguka: “KWA HAKIKA ALLAH
AMEWAPA RADHI WAISLAMU WALIPOFUNGAMANA NAWE CHINI YA MTI; NA ALIJUA YALIYOMO
NYOYONI MWAO. BASI AKATEREMSHA UTULIVU JUU YAO, NA AKAWAPA KUSHINDA KWA ZAMA
ZA KARIBU. NA NGAWIRA (nyara) NYINGI WATAKAZO ZICHUKUA, NA ALLAH NI MWENYE
NGUVU (na) MWENYE HIKIMA”. [48:18-19]
II.
Makureishi walegeza
msimamo wao na kuamua kukaa katika meza ya suluhu.
Khabari za baia hii
tukufu zikagonga ngoma za masikio ya Makureishi na kitendo hiki chenye
kuonesha upeo wa imani kikawaweka sawa na kuwarudishia busara pevu. Wakaanza
kuufikiria upya msimamo wao mkali na kulitazama suala hili kwa uoni wa mbali.
Wakaangalia nyuma, sasa na mustakbali (hali yao ya baadae) wao na jamaa yao
huyu Muhammad, mustakbali majuhuli (usiojulikana utakuwaje). Na pengine
walitafakari katika waliyo tafakari, kwamba hawa walioziuza nafsi zao kwa
Allah na kuyaendea mauti kwa mori na hamasa hii kubwa. Wakafanya hivyo wakiwa
katika hali ya udhaifu wa silaha/maandalizi na uchache wa idadi. Hawakuyafanya
yote haya ila wakiwa na yakini ya kupata nusra na ushindi kutoka kwa Allah kwa
kuwa wako juu ya haki. Na Makureishi walikuwa wanakiri kuwa waislamu wana haki
na hili walitakalo, yaani kuizuru nyumba ya Allah. Na kwamba wao wako katika
batili kwa kuwanyima haki yao hiyo, pia hawakupuuzia hata kidogo kwamba siku
zote Allah huinusuru haki na kuitupa mkono batili. Kwa hivyo basi lau wao
watapambana na waislamu, mapambano yakaisha kwa waislamu kuibuka na ushindi.
Basi huo ndio ungekuwa mwisho wa uongozi na utukufu wao miongoni mwa Waarabu
wenzao. Hali kadhalika Makureishi waliuona msimamo thabiti usiotetereka wa
waislamu na jinsi walivyokuwa tayari kuilinda imani yao hata kwa gharama ya
nafsi zao. Kwa hivyo ikawa ni lazima wawaidhike na kunasihika na hali halisi
waishuhudiayo na kuihisi kwa milango yao yote ya fahamu/hisia. Na waache
kiburi, jeuri, dhulma na upasito wao utokanao na kujiona.
Huenda Makureishi
waliyafikiria yote haya, wakaupima mwenendo na mtiririko wa mambo/matukio kwa
kugeuka nyuma kuangalia huko walikotoka. Hapa walipo hivi sasa na huko
waelekeako ambako hakuna akujuaye wala kubashiri kukoje. Na wakalinganisha
baina ya haki na batili katika msimamo wao na baina ya kheri (wema) na shari
(uovu) katika suala hili. Baada ya tafakari hizi za kina, ndipo ilipo
wadhihirikia kuwa suluhu ni bora zaidi kuliko kuendelea katika dhulma na uadui
usio na natija njema. Na kwamba kurudi katika haki ni bora zaidi kuliko
kuendelea kushikilia batili. Na kwamba kumili kwenye amani kutaibakisha haiba
na utisho wao kuliko vita ambavyo matokeo yake hayajulikani wala kutabirika.
Khususan pale walipoiona nia ya Wahabeshi na watu wa Thaqiyf kutaka kujitoa
katika ushirika wao. Kwa sababu ya kutokukubaliana kwao na msimamo wao huu wa
upasito kumuelekea Muhammad na maswahaba wake. Kwa kuyazingatia yote haya,
Makureishi wakaona ni kheri kuiitika mito ya amani itolewayo hata na washirika
wao wa karibu. Wakamtuma Suhail Ibn Amrou kuuongoza ujumbe wa watu kadhaa
kwenda kuongea na Muhammad juu ya suala zima la suluhu. Huku sharti kuu la
mazungumzo haya likiwa ni kumtaka Mtume arudi Madinah bila ya kuingia Makah
mwaka huu, ili kulinda heshima na kubakisha heba yao baina ya Waarabu.
|