Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

ABU JANDAL IBN SUHAIL

 Faida

       Kama kwamba Allah Taala alitaka kupima upeo wa subira na nguvu ya imani ya waumini. Akawapelekea Abu Jandal Ibn Suhail Ibn Amrou katika kitambo ambacho hata wino wa mkataba wa amani haujakauka. Akawajia akikimbia kutoka Makah akiwa na pingu za miguu na mikono. Huko Makah atokako alikuwa amefungwa katika nguzo ya chuma na baba yake; Suhail ambaye ndiye yuko mbele ya Mtume akiandika mkataba kwa niaba ya Makurayshi. Baba yake aliyetumwa kama mjumbe kwenda kuzungumza na Mtume, ndipo yeye alipopata upenyo akatoroka mahabusu akiwa na pingu zake. Akapita njia za uficho akipanda na kushuka majabali mpaka akafika Hudaybiyah. Waislamu wakampokea kwa shagwe na furaha, wakamtaka hali na kumuweka mahala apumzike kutokana na machofu ya safari ndefu. Suhail akainua kichwa chake akatupa jicho, akamuona mwanawe; Abu Jandal aliyemuacha Makah akiwa kifungoni kwa kosa la kusilimu na kuacha dini ya wazazi wake. Akamuinukia na kuanza kumshushia kisago cha nguvu, akamkwida barabara, Abu Jandal akapaaza sauti kutokana na kipigo kikali kilichokuwa kikimshukia: “Enyi kusanyiko la waislamu, hivi ninarejeshwa kwa mushrikina wanifitinishe na dini yangu?!”, kauli hii nzito inayogusa imani moja kwa moja ikawazidishia waislamu machungu juu ya machungu waliyokuwa nayo yaliyotokana na mkataba ule wa upande mmoja zaidi. Wakaanza kulia kutokana na maneno haya yenye hisia za imani yaliyotamkwa na ndugu yao wa imani; Abu Jandal. Suhail Ibn Amrou akamwambia Mtume wa Allah: “Hili ndilo suala la mwanzo nililo andikiana nawe mkataba, haya mrudishe. Wallah sitaendelea na mkataba mpaka umrudishe kwanza”. Mtume hakuwa na la kufanya ila kuutekeleza mkataba,  akamrudisha huku akimsihi amuachie. Lakini Suhail akaziba masikio, akayakataa maombi hayo ya Mtume na pale pale mbele yake na maswahaba akaanza kumpiga usoni na tawi la mti wa miiba. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akamwambia: “Nipe hiba kijana wako huyu au muokoe na adhabu hii”, Suhail akajibu: “Wallah, hilo silifanyi!” Baadhi ya wajumbe waliokuwemo katika ujumbe wa Suhail ndio waliomnusuru na suluba hiyo kali. Halafu ndipo Mtume wa Allah alipopaaza sauti yake na kusema: “Ewe Abu Jandal subiri na utarajie malipo (ya mateso haya) kutoka kwa Allah. Kwani hapana shaka Allah atakupa wewe na wanyonge wote walio pamoja nawe (huko Makah) faraja na muondokano wa dhiki zote hizi! Hakika sisi tumeshafunga mkataba na watu hawa, sisi tumewapa na wao wametupa ahadi ya Allah nasi hatuthubutu kuvunja tuliyokwisha yaridhia”.

Hamasa na mori vikampanda Sayyidina Umar Ibn Al-Khatwaab-Allah amuwiye radhi-na kumsukuma kwenda kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akamuuliza tena kama alivyomuuliza mwanzo. Kisha akamuendea Sayyidina Abu Bakri na kumuuliza pia, halafu akachupia kwa Abu Jandal; mteswa wa imani akitembea pembeni yake na kumwambia: “Subiri ewe Abu Jandal, hakika si vinginevyo hawa ni mushrikina tu na vyo vyote iwavyo damu ya mmoja wao ni mithili ya damu ya mbwa tu!” Akawa akimsogelea karibu na kumkurubishia mkono wa jambia akimtarajia auchukue na kumpiga nao baba yake, lakini Abu Jandal hakuweza kumuua baba yake. Akalazimika kukubaliana na matokeo ya imani yake mpaka pale Allah atakaposhusha faraja yake. Akarudi Makah vile vile akichechemea na pingu zake na huku waislamu wakimsindikiza kwa macho ya huzuni na masikitiko makubwa. Macho yao yakafurika na kububujika machozi ya huruma kwa kutokuwa na njia ya kumuokoa.

 

     V.          Waislamu wagubikwa na huzuni kiasi cha kukurubia kuuana wao kwa wao:

          Suhail na ujumbe wake walipomaliza kuandika mkataba na kushika njia wakaondoka, Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akawaambia maswahaba wake: “Inukeni, mchinje, mnyoe na mfungukane na ihramu yenu”. Hapana hata mtu mmoja aliyeiitikia amri yake hiyo, akayakariri tena maneno yake hayo mara tatu, lakini wapi bado hakuna aliyeinuka kutekeleza. Mtume akaingia hemani kwa mkewe; Ummu Salamah akiwa amewiva kwa ghadhabu, mkewe akamuuliza: “Kulikoni ewe Mtume wa Allah?”, Mtume akamjibu: “Waislamu wameangamia, nimewaamrisha hawakuamrika!”, halafu akamtajia hali aliyokutana nayo kwa maswahaba wake. Mkewe akamwambia: “Ewe Mtume wa Allah! Usiwalamumu, kwani hakika wao wamefikwa na jambo kubwa mno kutokana na mashaka uliyo jitumbukiza katika suluhu hii, na suala hili la kurejea bila ya kupata walilolijia limewahemeza”. Halafu ndipo mama huyu wa waumini alipomshauri atoke bila ya kuzungumza na ye yote, amchinje ngamia wake wa sadaka na anyoe nywele. Basi Mtume akatoka bila ya kuzungumza na mtu kama alivyoshauriwa, akamchinja ngamia wake na akamuita kinyozi wake akamnyoa. Watu walipomuona Mtume akifanya hivyo, nao haoo wakainuka wakachinja na wakaanza kunyoana mpaka wakafikia kukurubia kuuana wenyewe kwa wenyewe kutokana na huzuni kuu.

Abdullah Ibn Umar na Abdullah Ibn Abbas-Allah awawiye radhi-wamesema: “Watu walinyoa siku ile ya Hudaybiyah na wengine walipunguza tu, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema: “Allah awarehemu walionyoa”, maswahaba wakasema: Ewe Mtume wa Allah na waliopunguza je? Akasema: “Allah awarehemu walionyoa”, wakasema tena: Ewe Mtume wa Allah na waliopunguza je? Akasema tena (kwa mara ya tatu): “Allah awarehemu walionyoa”, wakasema maswahaba (mara ya tatu): Ewe Mtume wa Allah na walio punguza je? Mtume akasema: “Na waliopunguza (Allah awarehemu pia)”. Wakauliza: Ewe Mtume wa Allah wee! Ni kwa nini umewakhusu walionyoa kwa rehema na kuwaacha nyuma waliopunguza? Akajibu: “Kwa sababu wao hawakuitilia shaka amri yangu”.

 

Ushindi bayana:

       Pamoja na kwamba waislamu waliuitikia wito wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakawachinja wanyama wao wa sadaka na wakafungukana na ihramu zao. Lakini bado wao walikuwa katika muhemezo kulielekea suala hili la suluhu aliyoipitisha Mtume bila ya ridhaa/kinyume na matakwa yao. Akaipitisha pamoja na dhulma na punjo la wazi lililokuwemo humo, mpaka wakafikia kumuuliza Mtume juu ya ile bishara ya kuingia msikiti mtukufu aliyowapa. Kisha isitimie, kwani wanarudi Madinah bila ya kutufu  Al-Ka’abah, nae Mtume akiwauliza: “Kwani mimi nilikuambieni kuwa mtaingia mwaka huu (au nilisema tu mtaingia)?”, nao wakijibu: “Hapana (hukusema mwaka huu)”. Ndipo alipowaambia: “Basi bila ya shaka mtaingia (humo) na mtafanya twawafu, inshallah”, nao wakizidi kumuuliza: “Na jinsi gani tumrudishe kwa makafiri mtu aliyetujia hali ya kuwa muislamu na wala wao wasilazimike kuturudishia mtu aliyewaendea hali ya kuwa murtadi?”, Mtume akiwaambia: “Ye yote miongoni mwetu atakayekwenda kwao, basi Allah asimrejeshe na atakayetujia kutoka kwao nasi tukamrejesha (kwa ajili ya kutekeleza mkataba). Basi hapana shaka kuwa Allah atamjaalia faraja na mapito ya kutokana na dhiki (ya makafiri)”. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akakaa Hudaybiyah kiasi cha siku kumi na kitu. Halafu tena huyoo akashika njia kurudi Madinah, wakati akiwa njiani ndipo Allah alipomteremshia Suratil-Fat-hi [48]. Watu wakaja wangu wangu mpaka wakamkusanyikia, akawasomea: “BILA SHAKA TUMEKWISHAKUPA KUSHINDA KULIKO DHAHIRI”. [48:01]. Umar akauliza: “Hivi huu ndio ushindi ewe Mtume wa Allah?!”, (Mtume) akajibu: “Naam, namuapia yule ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake, hakika huo ni ushindi”. Mmoja wa maswahaba akarukia na kusema: “Huu sio ushindi kitu, watu tumezuiliwa na nyumba ya Allah na wanyama wetu pia wamezuiliwa. Na kisha tena Mtume wa Allah amewarejesha kwa makafiri waumini waliomjia (huu ndio ushindi huu)?”. Kauli ya mtu huyu ikamfikia Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akasema: “Ni maneno mabaya yaliyoje hayo! Basi huu ni ushindi mkubwa kuwahi kutokea, hakika mushrikina wameridhia kukuzuilieni kwa kutoingia mjini kwao (bila ya kutumia njia ya vita). Tena wamekujilieni kujadiliana nanyi juu ya suala la suluhu na kukuraghibishieni amani ilhali wameyaona kwenu yawachukizayo. Nae Allah akakushindisheni juu yao na akakurejesheni mkiwa salama na ilhali mmepata ujira (wa nia yenu ya Umrah), basi huu ndio ushindi mkuu nyinyi kuwahi kuupata. Hivi mmekwisha sahau siku ile ya vita vya Uhud mlipokuwa mkikimbia mbio, wala hamumsikilizi ye yote ilhali mimi nikukuiteni nikiwa nyuma yenu?! Hivi mmekwisha sahau pia siku ya vita vya Ahzaab pale walipokujieni kukushambulieni kutokea juu yenu na kutoka chini yenu. Na macho yalipokodoka na nyoyo zikapanda kooni, nanyi mkaanza kumdhania Allah dhana mbali mbali?”. Waislamu wakasema: “Amesema kweli Allah na Mtume wake! Huu wallah ndio ushindi mkuu kuliko yote, ewe Mtume wa Allah. Sisi hatukuyafikiria kamwe uliyoyafikiria, wallah wewe unamjua mno Allah na mambo yake kuliko sisi”. Naam, hivi ndivyo waislamu walivyorejea kutoka Hudaybiyah, nyoyo zao zikiwa zimetua na kukwatuka na wakayakinisha kuwa Allah amewatakia kheri katika suala hili la suluhu. Lakini bado walikuwa hawajui kheri hii itatoka wapi, lini na vipi.

 

 



 | Tuandikie |