|
SOMO LA KWANZA.
I.
Huenda mkalichukia jambo
na Allah akajaalia kheri nyingi ndani ya jambo hilo.
Waislamu hawakupata katu kuwa na msimamo dhidi ya Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-kama waliokuwa nao katika suluhu ya
Hudaybiyah. Na wala hawakutokea kumpinga kwa lo lote kama walivyompinga katika
suluhu hii waliyoiona kuwa imeegemea zaidi upande mmoja. Na Mtume kwa upande
wake hakupata kushika msimamo uliowaudhi na kuwakera kuliko huu, kwani
aliipitisha suluhu kinyume kabisa na matakwa yao. Na akaacha kuwataka ushauri
katika suala hili tete kama alivyo wazoesha ikiwa ni amri kutoka kwa Mola
wake. Na akaukabili ushindani na upasito wa Makureishi kwa upeo wa wepesi na
ulaini. Isitoshe akamrejesha adhabuni na fitinani Abu Jandal wakati ambapo
mkataba wa amani ulikuwa haujasainiwa bado kuashiria kuwa umepitishwa na
kuridhiwa na pande zote mbili.
Waislamu katika siku hii wakawa na hisia za unyonge na
kudhalilishwa, nafsi zao zikachemka kwa hisia kali za utukufu wa imani na
nguvu ya mshikamano wa haki. Mpaka Umar Ibn Al-Khatwab-Allah
amuwiye radhi-akafikia kujadiliana na Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akionyesha upinzani na chuki ya wazi. Akiuliza kwa mshangao sababu
iliyompelekea Mtume wa Allah kuukubali unyonge na uduni huu. Nae Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akimjibu kwa utulivu uliosheheni kujiamini na
kuelewa asemacho, akimwambia: “Mimi ni mja na mjumbe wa Allah, sitaikhalifu
amri yake na wala yeye hatanitupa na kuniacha”. Hapa sasa ndipo ulipo muhimili
unaozungukia kadhia yote hii, kwani ni wazi kuwa maamuzi yote aliyoyachukua
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-ulikuwa ni wahyi (ufunuo) kutoka kwa
Allah Mola Muumba wake. Kwa lugha nyepesi tunaweza kusema aliyafanya yote
aliyoyafanya na katu hakuyafanya kwa matashi ya nafsi yake. Kwa ajili hii
basi, hakukumfalia wala kumpasia yeye kwenda kinyume na amri ya Mola wake
ambaye aliyemnusuru na kumuunganishia nyoyo za waumini. Na wala hakupaswa
kuwataka ushauri maswahaba wake au kufuata maono na fikra zao katika hili na
ilhali tayari amekwisha pewa amri kutoka kwa aliye juu ya kila kitu na mwenye
busara. Na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alilihisi hili tangu
mwanzoni kabisa pale ngamia wake alipokita magoti kwenye maporomoko ya bonde
la Hudaybiyah na maswahaba wake wakasema: “Ameasi/amefanya ukorofi”. Nae
akawaambia: “Hajaasi, lakini kilichomzuia ni kile kile kilichomzuia kuingia
Makah ndovu (wa Aburahah)”. Na tangia hapo ndipo Mtume akaiandaa nafsi yake
kukubali kila hatua inayopelekea kwenye amani na suluhu. Muda wa kuwa msingi
wake ni kuyaadhimisha matukufu ya Allah na akaitangaza nia hii njema wazi wazi
pale aliposema: “Namuapia yule ambaye nafsi yangu imo mikononi mwake, leo
Makureishi hawataniitia hatua ambazo watayaadhimisha ndani yake matukufu ya
Allah. Na ndani yake kuna kuunga udugu ila nitawaitikia”. Sasa pale ilipo
mdhihirikia nia ya Makureishi kutaka suluhu, hakusita kuipokea na kuikubali
nia yao hiyo na kuanza kuifanyia kazi mara moja. Na akafanya nia yake ni
kulifikia lengo hili hata kama kufanya kwake hivyo kutamtumbukiza miibani. Na
kwa mtazamo wake lengo hili lilikuwa tukufu na thamani mno kuliko kupotea kwa
sababu tu ya maneno ya uchokozi/kukirihisha na mandhari ya ukavu na ugumu wa
nyoyo. Ni kwa ajili hii ndio hakuupatiliza upuuzi wa Makureishi katika kadhia
hii ya amani. Na akamchukulia mjumbe wao upeo wa kumchukulia kiasi cha kuonwa
na maswahaba amekuwa laini mno na kuyakubali matakwa yote ya mahasimu wao.
Wala hakuangaishwa na kushughulishwa na mori wa hasira uliowapanda maswahaba
wake kutokana na kuridhia kwake kwa kifua kikunjufu ugumu na inadi ya mahasimu
wao. Akaendelea na kadhia hii, akiishughulikia kwa hekima/busara na siasa yake
makini. Mpaka ikafikilia tamati yake njema akitaraji kwayo kheri kwa Uislamu
na waislamu. Kama kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa
akiangalia kwa jicho la ghaibu kilichoko upande wa pili/nyuma ya suluhu hii.
Suluhu ambayo ilitazamwa na maswahaba kuwa ni kukubali unyonge na kudunishwa
katika imani yao ya kweli.
Kwa kweli suluhu hii ilitoa matunda yake haraka mno kuliko
ilivyo tazamiwa na waislamu. Na ilileta natija ya kushangaza mno kuliko ilivyo
sawirishwa katika fikra na maono yao. Na matunda yake yalikuwa mazuri mpaka
Allah Taala mwenyewe akayaita kuwa ni: “USHINDI ILIO DHAHIRI (bayana)”, kama
kwamba ushindi huu bayana ulikuwa ni mlango ulioficha kheri nyuma yake au ni
kizuizi kinachozuia mafuriko. Mlango/kizuizi hiki kilipofunguka kheri
ilichimbuka mchimbuko wa kasi na enevu. Hivi ndivyo Allah Taala
anavyolizungumzia tukio zima la suluhu hii ya Hudaybiyah: “BILA SHAKA
TUMEKWISHAKUPA KUSHINDA KULIKO DHAHIRI. ILI ALLAH AKUSAMEHE MAKOSA YAKO
YALIYOTANGULIA NA YANAYOKUJA, NA KUTIMIZA NEEMA ZAKE NA KUKUONGOA KATIKA NJIA
ILIYO NYOOKA. NA AKUNUSURU ALLAH NUSURA YENYE NGUVU KABISA... ALLAH
ANAKUAHIDINI NGAWIRA (nyara) NYINGI MTAKAZO ZICHUKUA; KISHA AMEKULETEENI HAYA
KWANZA (kabla ya hayo) NA AKAIZUIA MIKONO YA WATU ISIKUFIKIENI, NA ILI IWE
DALILI (ya kheri) KWA WAUMINI NA KUKUONGOZENI NJIA ILIYO NYOOKA. NA (atakupeni
ngawira) NYINGINE, HAMJAWEZA KUZIPATA BADO, (ambazo) ALLAH AMEKWISHA ZIZINGIA,
NA ALLAH NI MUWEZA WA KILA KITU”. [48:1-3, 20 & 21]
|