Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

II. VITA IKASITISHWA NA DA'WAH IKAPATA NJIA

 Faida

          Ikawa katika jumla ya matunda ya suluhu hii, ni kusitishwa kwa vita baina ya waislamu na Makureishi. Ni vema ikakumbukwa kwamba hawa Makureishi ndio waliokuwa kikwazo kikubwa tangu kudhihiri kwa Uislamu. Na uadui na chuki zao dhidi ya Uislamu na waislamu ukawa ndio chemchem na shina la mabalaa yote yawafikayo waislamu. Na Waarabu wengine na Mayahudi nao wakawa wanafuata nyayo za Makureishi katika kuhakikisha kuwa Uislamu unakufa. Kama kwamba Makureishi ndio waliokuwa kijinga cha moto kinachowasha moto wa uadui na chuki dhidi ya waislamu. Ilipotimia suluhu baina yao na waislamu, kijinga hiki hatari kikawa kimezimika chenyewe. Na hivyo kuufanya moto ukizungukao kugeuka na kuwa majivu yasiyomdhuru hata mdudu chungu. Tumeona hukoo tulikoanzia kwamba mara tu Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipoanza kuitekeleza amri ya kufikisha ujumbe wa Allah kwa waja wa Allah. Hapo hapo Makureishi nao wakaingia kazini na kutangaza vita dhidi yake ikiwa hatoacha kuendelea kuitangaza imani hiyo ya Mungu mmoja. Wakamuwekea vikwazo vya kila namna ili tu asiweze kufanikiwa kupata wafuasi. Wakati mwingine wakatumia propaganda na kueleza kuwa yeye ni mchawi, mara kuhani, mara mwendawazimu na mara nyingine wakisema kuwa ni muongo. Wakiwatahadharisha watu katika misimu ya Hijah na Umrah dhidi ya shari na uchawi wake ili wapate kumtenga. Mpaka wakafikia kumuweka yeye na watu wake katika vikwazo na kuhakikisha kuwa hakuna kiingiacho wala kutoka kwao mpaka wasalimu amri. Vikwazo hivi vilikaribia kuwaua kwa njaa na isitoshe waliwabadilishia maswahaba wake anuwai za adhabu. Kiasi cha kufikia kuwatoa kwa nguvu majumbani mwao na kuwanyang’anya mali zao. Na wakala njama za kumuua Mtume mpaka wakamlazimisha kuhamia Madinah na huko bado wakaendelea kumfuata na kumshambulia. Wakishirikiana na Mayahudi wa Madinah kufanya majaribio kadhaa ya kumuua na wakimkusanyia majeshi shirika na kumuundia makundi ya kumuangamiza. Matukio mfululizo muambatano haya yasiyokoma, ndiyo yaliyoyafanya maisha ya Mtume na maswahaba wake kuwa ni jihadi endelevu na mapambano ya nguvu.

Kisha tena hawa hawa Makureishi baada ya kibri na inadi yao, baada ya upinzani wao usiochoka na uadui wao mkali. Sasa wamekuja kukaa na mahasimu wao hawa katika meza moja ya mazungumzo wakitaka kusimamishwa vita na kupatikana amani baina ya pande mbili hizi. Wakiikubali wenyewe amani baada ya kuikataa huko nyuma na kumtuma mjumbe wao kwenda kujadiliana na Mtume juu ya suala la suluhu. Kuna fursa gani nyingine iliyokuwa nzuri kuliko hii kutumiwa na Mtume wa Allah kwa maslahi ya Uislamu na waislamu?! Fursa itakayofungua ukurasa mpya kwa mlingano (da'awah) wa Uislamu ambao Mtume amekuwa akipigania kusimama kwake. Kwa yakini, hii ilikuwa ni fursa adhimu na adimu ambayo ni khasara tupu kuipoteza. Na ni fursa ambayo haikupaswa kuzuiwa na kupotezwa kwa sababu ya mambo ya kipuuzi yaliyojitokeza. Khususan upande wa Makureishi uliotia mkazo usio na maana zaidi ya kuonyesha jeuri yao iliyofurutu ada. Kwa hakika Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliitumia vema fursa hii, akaupitisha mkataba wa amani baina yake na Makureishi. Tena akaipitisha suluhu kama walivyotaka Makureishi, bila ya kujali ghadhabu ya maswwahaba wake wala ujinga/upuuzi wa Makureishi na tashdidi zao. Kwa kitendo chake hiki kitukufu chenye kusifiwa na kufanywa kuwa ni ruwaza/kigezo chema kwa kila kiongozi wa uma. Akawa amepiga na kusajili mfano bora kabisa katika medani ya siasa, hekima na diplomasia. Na hapo hapo akawa ameonyesha uwezo wake mkubwa katika kuyachunguza mambo na umahiri wake mpana katika kuangalia natija/matokeo ya mambo.

 

      III.          Waislamu wakawa na uwezo wa kuwasiliana na watu katika vitongoji vyao na kuwafikishia ujumbe wa Allah bila ya bughudha.

          Katika jumla ya matunda bivu ya suluhu hii ni kufunguka uwanja wa kazi ya da'awah kwa waislamu na hivyo kuwafagilia njia ya kuzifikia nyoyo za walengwa. Kwani baada ya kuwa waislamu wamefungika Madinah peke yake, hawana fursa ya kufikisha ujumbe nje ila kwa uficho mkubwa. Wakiwa wamekatiwa mawasiliano na makabila ya Kiarabu yale yaishiyo mjini na yale ya mashambani. Kwa kupita na kuridhiwa suluhu na pande mbili hizi hasimu, sasa kukawamkinikia waislamu kuwa na mawasiliano ya moja kwa moja na watu katika vitongoji vyao. Na wakaweza kukutana na kuchanganyika na watu katika sehemu/makazi yao na kuwafikishia ujumbe wa Allah. Wakiwafafanulia misingi ya dini hii ya haki na ukweli na hakika ya wito wake na kuwaonyesha misingi ya utu na tabia njema zinazolinganiwa na dini hii. Watu kutokana na hali na matendo ya waislamu wanayoyashuhudia na mwenendo wa Mtume wanaousikia na kuuona kwa macho yao wenyewe. Wakaanza kuujongelea, kuukubali na hatimaye kuukumbatia Uislamu baada ya kuona uzuri wa misingi na mafundisho yake kupitia kauli na amali za waislamu na Mtume wa Uislamu. Kwa njia hii, Uislamu ukatangaa na kuenea kwa kasi katika makabila ya waarabu na watu wengi wakaupokea kama njia ya maisha yao na imani yao ya uwokovu. Mzingo na wigo wa Uislamu ukazidi kutanuka siku hata siku mpaka Makah yote ikawa imesilimu na kuikubali haki. Nayo idadi ya waislamu ikazidi kuongezeka na kurudufika, kiasi haikupita miaka miwili tangu kumalizika kwa tukio la Hudaybiyah. Mpaka Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaingia Makah akiwa na kundi la maswahaba wasiopungua elfu kumi. Wakati ambapo siku ile ya Hudaybiyah jeshi lake halikuwa na askari zaidi ya elfu moja na mia sita.

Kama alivyojishughulisha Mtume na jukumu la kuutangaza na kuueneza Uislamu katika miji ya Waarabu. Ndivyo hivyo hivyo alivyochukua juhudi ya kuueneza katika falme na nchi zilizomzunguka. Akawaandikia ujumbe rasmi viongozi na wafalme wa nchi hizo, akiwalingania Uislamu. Akawateua na kuwakabidhi kazi hii ya kufikisha ujumbe kwa wafalme na viongozi hawa watu mahiri miongoni mwa maswahaba wake. Akawatuma mtu mmoja, barua moja kwa mfalme mmoja, pamoja na ukweli kwamba wengi wa wafalme na viongozi walengwa hawa kutozipokea vema barua za Mtume wa Allah bali hata hao wajumbe wa Mjumbe wa Allah. Bado sauti ya uislamu ilifika na kurindima katika nchi hizo mpaka Allah akazitiisha na kuupokkea Uislamu katika kipindi kisichozidi miaka thelathini.

 



 | Tuandikie |