|
IV.
Suluhu ya Hudaybiyah
yawakasirisha Mayahudi na kuamua kuvunja ushirika wao na Makureishi.
Miongoni mwa matunda matamu yaliyopatikana kutokana
na kuupanda mti wa amani wa Hudaybiyah. Ni kule Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-kuutua mabegani mwake mzigo wa kuwafikiria Makureishi. Na badala
yake akazielekezea nguvu zake zote kwa Mayahudi ambao ndio waliokuwa adui
nambari mbili nyuma ya Makureishi. Hawa waliendelea kutumia njia zao za hila
na vitimbi na mbinu chafu kuzidhoofisha nguvu za Uislamu na kuzivunja nguzo
zake. Mpaka dola ya Kiislamu isisimame na wala waislamu wasiwe na sauti/nguvu.
Tegemeo lao la kwanza katika kuzitekeleza dhamira zao chafu hizi na kuyafikia
malengo duni yao haya, lilikuwa ni Makureishi. Na la pili yalikuwa ni makabila
ya Waarabu waliokuwa jirani nao. Sasa basi, ilipofikiwa na kuridhiwa suluhu
baina ya Waislamu kwa upande mmoja na Makureishi kwa upande wa pili. Na
miongoni matokeo ya suluhu hii ikawa ni kusitishwa kwa vita baina ya pande
mbili hizi kwa kipindi maalumu. Ambacho hicho kitakuwa ni kipindi mpito cha
amani, hili likayavuta makabila mengine ya Waarabu kutaka amani. Mayahudi
wakawa kama kwamba wametengwa na washirika wao (Waarabu) dhidi ya hasimu wao
mkubwa Muhammad. Mtandao wao dhidi ya Mtume na waislamu ukawa finyu kuweza
kutoa upinzani wa haja. Hapa ndipo waislamu walipoamua kutoipoteza fursa hii
adimu, wakajiandaa kuitumia vema fursa hii ya dhahabu kwa maslahi ya Uislamu
na Waislamu. Wakafanya maandalizi ya kutosha kumfagilia mbali adui huyu
msaliti mwenye vitimbi. Adui isiyoaminiwa shari yake iwezayo kuripuka na
kuhatarisha usalama wao wakati wo wote. Adui isiyotarajiwa kheri yake kuwa iko
siku atakuwa na matangamano na mahusiano mema na jirani zake. Hapo ndipo
yalipofuatana matukio kama yale ya Khaybar, Fadaka, Taymaa na kwingineko.
Kupitia matukio hayo, Allah akautia nguvu na kuupa ushindi Uislamu na
kumdhalilisha na kumtenza nguvu adui huyu muovu.
SOMO LA
PILI.
I.
Makureishi waikiri haki
ya waumini kuizuru nyumba ya Allah.
Katika jumla ya natija njema zilizotokana na suluhu
hii, ni Makureishi kuikiri haki ya waislamu kufanya ziara katika nyumba ya
Allah. Na kwamba hili lifanyike na kutimia chini ya mazingira ya amani bila ya
vita. Huku kukawa ni kufuzu kukubwa kwa Waislamu Madinah na kheri na baraka
kwa waislamu wanyonge waliokuwa Makah. Kwani huko Makah walikuweko waislamu
wake kwa waume wasiotambuliwa na Mtume na hata maswahaba wake. Hawa walikuwa
ni miongoni mwa hao wanyonge wasioweza kuitangaza wazi imani yao. Na wala
hawana njia wala upenyo wa kukimbia kutoka Makah kwenda Madinah kwa ajili ya
dini yao. Lau basi vita vingeliuma baina ya pande mbili hizi, hapana shaka
kwamba wengi wa wanyonge hawa wangelikuwa miongoni mwa wahanga wa vita hivi.
Na waislamu wangeliwaua ndugu wao hawa wa imani pasina kuwajua na hili
likawatia khasarani kwa kuwapoteza ndugu zao hao, tena kwa mikono yao wenyewe.
Hivi ndivyo Allah Taala anavyolitaja hili kwa njia ya kumsumbulia na
kumkumbusha neema hiyo Mtume wake na waumini wote kwa ujumla. Haya na tusome
kwa mazingatio: "NA YEYE NDIYE ALIYEIZUIA MIKONO YAO KWENU, NA MIKONO YENU
KWAO, KATIKA BONDE LA MAKAH BAADA YA KUKUPENI (Allah) USHINDI JUU YAO. NA
ALLAH ANAONA (yote) MNAYOYATENDA. HAO NDIO WALIOKUFURU NA WAKAKUZUILIENI
KWENDA KATIKA MSIKITI MTUKUFU (wa Makah baada ya kukaribia hapo kwa kiasi cha
maili 48). NA WAKAWAZUILIA WALE WANYAMA (mliowachukua kwa ajili ya kuchinjwa)
WASIFIKE MAHALA PAKE. NA LAU KAMA SI WANAUME WAUMINI NA WANAWAKE WAUMINI
(walioko Makah wanaficha Uislamu wao), MSIOWAFAHAMU MSIJE MKAWASAGA BILA
KUJUA, NA KWA HIVYO MKAPATA MASIKITIKO KWA AJILI YAO (ingalikuwa si haya,
Allah asingekuzuieni kupigana nao. Amefanya haya) ILI ALLAH AMUINGIZE AMTAKAYE
KATIKA REHEMA YAKE. KAMA (waislamu na makafiri) WANGALITENGANA BILA SHAKA
TUNGELIWAADHIBU WALE WALIOKUFURU MIONGONI MWAO ADHABU IUMIZAYO. PALE WALE
WALIOKUFURU WALIPOTIA NYOYONI MWAO MORI, MORI WA UJINGA; BASI HAPO ALLAH
ALITEREMSHA UTULIVU WAKE JUU YA MTUME WAKE NA JUU YA WAISLAMU. NA
AKAWALAZIMISHA NENO LA KUMCHA ALLAH; NAO WALIKUWA NDIO WENYE HAKI ZAIDI NALO
NA WALIOSTAHILI. NA ALLAH NI MJUZI WA KILA KITU. KWA YAKINI ALLAH
AMEMUHAKIKISHIA MTUME WAKE NDOTO YAKE YA HAKI. BILA SHAKA NYINYI MTAINGIA
KATIKA MSIKITI MTUKUFU INSHA-ALLAH KWA SALAMA MKINYOA VICHWA VYENU NA
MKIPUNGUZA NYWELE (kama ilivyo wajibu kufanya hivyo wakati wa Hijah).
HAMTAKUWA NA HOFU (wakati huo) NA (Allah) ANAJUA MSIYOYAJUA. BASI KABLA YA
HAYA ATAKUPENI KUSHINDA (kwanza) KULIKO KARIBU (kuwashinda Mayahudi)".
[48:24-27]
|