Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

II. MAKURESHI WAOMBA MSAADA WA MTUME WA ALLAH

 Faida

Miongoni mwa yaliyokuwa masharti ya mkataba ule wa amani wa Hudaybiyah lilikuwepo sharti moja lililowatia uchungu mno waislamu. Na kwa upande wa pili Makureishi waliling'ang'ania mno. Sharti hili kwa rehema zake Allah likageuka na kuwa faraja na mlango wa kutokea katika dhiki wa waislamu wanyonge walioko Makah. Na likawa mwiba mchungu kwa mushrikina waliokamatana nalo na kulisisitiza kupindukia. Sasa ikawa wao ndio wanaoendesha juhudi za kutaka lifutwe sharti hili katika mkataba. Na walitangaza wazi kujivua nalo hata kabla ya mwaka mmoja tangu kuzaliwa kwa mkataba ule. Hili lilianza pale Abu Busweir; Utbah Ibn Usayd At-thaqafiy alipokimbilia Madinah akitokea kwa Makureishi waliokuwa wakimuadhibu na kumtesa kwa sababu tu ya imani yake. Huku nyuma Makureishi wakawatuma watu wawili kwenda kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Kumtaka amrejeshe kwao mtu wao huyo, ikiwa ni katika jumla ya kulitekeleza mojawapo ya masharti ya mkataba baina yao. Mtume wa Allah alipojiwa na ujumbe huo akasema: "Ewe Abu Busweir, hakika bila ya shaka sisi tumeshawapa watu hawa kile unachokijua na wala haitufalii sisi katika dini yetu kufanya usaliti. Kwa ajili hii basi, rudi kwa watu wako". Abu Busweir akasema: Ewe Mtume wa Allah! Hivi unanirudisha kwa mushrikina wanifitinishe na dini yangu?", Mtume akamwambia: "Nenda, kwani hapana shaka Allah atakupa wewe na wanyonge wote walio pamoja nawe faraja na mlango wa kutokana na dhiki na taabu mzipatazo". Hapo tena Abu Busweir hakuwa na hila ila kuondoka na kurudi Makah na wajumbe wawili wale waliotumwa kumrejesha. Akaenda nao hata walipofika mbali hukoo, akafanya hila na kufanikiwa kuutwaa upanga wa mmoja wa watu wawili wale. Akampiga na kumkatakata nao mpaka akamuua, mwenziwe kuona yaliyomfika tim akatimua mbio bila ya kuangalia nyuma kujiokoa na kifo dhahiri. Mbio zake hizo zikakomelea kwa Bwana Mtume, akiwa anatweta na kuhema kama bata akasema: "Mtu  wenu amemuuua mwenzangu",. Abu Busweir  akaja nyuma yake, akamtolea salamu Mtume kisha akasema: "Imetekelezeka dhima yako ewe Mtume wa Allah  na Allah amekutekelezea. Umenisalimisha kwa watu hawa na ilhali nimejuzuia kufitiniwa dini yangu". Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akamwambia: "Nenda utakako (lakini sio hapa)". Abu Busweir alipotoweka machoni, Mtume wa Allah akasema: "Ole wa mama yake, hiyo ni fimbo ya chuma ya kuchokolea moto lau angelikuwa na watu!"

Abu Busweir akaenda mpaka akapiga kambi katika sehemu fulani ya mwambao wa bahari, baina ya "Iyswi" na "Dhul-Marwah" katika ardhi ya Juhaynah. Akakaa hapo na kazi yake ikawa ni kuivizia misafara ya biashara ya Makureishi ipitayo njia hiyo. Kila msafara uliopita mahala hapo aliushambulia na kupora mali na chakula. Waislamu wanyonge waliokuwa Makah walipozisikia khabari za Abu Busweir na maneno aliyoambiwa na Mtume. Wakaanza kuchomoka kwa uficho mkubwa na kwenda kujiunga na Abu Busweir kwenye kambi yake hiyo. Abu Jandal naye akafanikiwa kutoroka Makah na kwenda kujiunga na wenzake hao akiwa analiongoza kundi la watu sabini wapamda wanyama waliosilimu. Watu wa makabila ya Ghaffar, Aslama na Juhaynah na makundi ya mabedui nao wakaja kujiunga na waislamu hawa katika kambi hii iliyoanzishwa na Abu Busweir. Mtu ambaye Mtume alishindwa kumpokea Madinah kutokana na kufungwa (kubanwa) na mkataba wa amani wa Hudaybiyah, nae asikubali kurudi adhabuni na kifungoni Makah. Kambi yake hii sasa ikawa na watu wasiopungua mia tatu na ili waweze kuendelea kuishi hapo, wakalazimika kuvamia na kupora misafara ya biashara ya Makureishi ipitayo hapo. Haupiti msafara hapo ila hutwaa mali yote na kuwaua watu wa msafara ule walioshindwa kuponyoka na kukimbia.

Kambi hii ya Abu Busweir ni zao na kivuno kilichotokana na masharti magumu ya suluhu waliyoyaweka Makureishi, ikawa ni mwiba mchungu uliowakalia kooni Makureishi. Wakahemewa wasijue la kufanya ila kupeleka ujumbe kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakimuomba kwa udugu wao awasaidie kutatua tatizo hili. Wakasema: "Sisi hatuna haja tena na watu hao, ye yote atakayetoka kwetu kuja kwako, basi sasa mzuie (kuwa nae) na hutakuwa na kosa (kufanya hivyo)". Hapo ndipo Mtume wa Allah alipoandika barua kumpelekea Abu Busweir na Abu Jandal akiwaamuru kwenda kwake. Na akiwaamuru waislamu walio pamoja nao kurejea makwao na wala wasizuie msafara wo wote wa Makureishi utakaopita hapo.

 

III.            Busara na weledi wa Mtume wa Allah katika mambo/mipango:

          Hivi ndivyo mambo yalivyokuwa, kadri siku zilivyopita ndivyo busara na weledi wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-ilivyobainika. Siasa yake makini na uoni wake wa mbali ulivyodhihirika na kuwakinaisha maswahaba wake na kuwaonyesha kwamba wao walifanya haraka kuichukia suluhu ile. Suluhu iliyoleta baraka, kheri na fanaka tupu kwa Uislamu kama dini na mfumo kamili wa maisha na waislamu wenyewe. Na ikawadhihirikia wale waliokimwa na suluhu hii kwamba Mtume wa Allah alikuwa sahihi na aliona mbali kuliko wao. Na kwamba alikuwa na yakini thabiti kwamba Allah Taala hatomtupa mkono na maono yake ndio yaliyokuwa na kheri kathiri na kufuzu adhimu.

Sayyidina Abu Bakri-Allah amuwiye radhi-alikuwa akisema: "Haukuwahi kupatikana ushindi mnono katika Historia ya Uislamu kuliko ule wa Hudaybiyah. Lakini watu siku hiyo, fikra zao zilishindwa kuyafikia yaliyokuwa yakijiri baina ya Muhammad na Bwana Mlezi wake. Na waja hufanya haraka na ilhali Allah hafanyi haraka kama wafanyavyo waja, mpaka mambo yafikie pale alipopataka. Kwa yakini nilimuona Suhail Ibn Amrou katika Hijjatul-Wadaai akiwa amesimama mahala pa kuchinjia wanyama. Akimsogezea Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-ngamia wake, nae Mtume akimchinja kwa mkono wake. Kisha akamuita kinyozi, akaja akamnyoa, nami nikimuangalia Suhail akiziokota nywele za Mtume na nikimuona anaziweka machoni kwake. Hapo nikakumbuka namna alivyokuwa akikataa siku ile ya Hudaybiyah kuandikwa "BISMILLAAHIR-RAHAMAANIR-RAHIYM". Na namna alivyopinga kwa nguvu zote kuandikwa "Muhammad Mtume wa Allah". Basi nkamuhimidi Allah aliyemuongoza kwenye Uislamu, naomba Rehema na Amani imshukie Mtume wa Rehema. Ambaye kwaye ametuongoza na kutuokoa na hilaki".

 



 | Tuandikie |