Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

III. MTUME AJARIBU KUISHI KWA AMANI NA MAYAHUDI

 Faida

III.            Mtume wa Allah ajaribu upeo wa juhudi yake kuishi kwa amani na Mayahudi , lakini maumbile yao ya usaliti yaliwashinda.

Hivi ndivyo yalivyokuwa maisha baina ya Mayahudi na majirani zao waislamu, yalikuwa ni mrorongo wa chuki na mifundo isiyopoa wala kukatika. Pamoja na yote haya, bado Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-hakupenda kujibu uhasama huu wa Mayahudi. Wala hakutaka kulipa uadui atendawao kwa uadui mfano wake, bali alikuwa akitafuta sana fursa itakayo muwezesha kuleta suluhu baina yake na wao ili waweze kuishi kwa amani na usalama. Na kamwe Mtume hakuanza kuwafanyia uadui, bali alifanya kila juhudi iliyokuwa ndani ya uweza wake kuwaita katika meza ya amani, mapenzi na ushirikiano.

Wakati uongozi wa Mayahudi katika Khaybar ulipotwaliwa na Useir Ibn Razaam na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akatambua kwamba anafanya maandalizi ya vita. Akaonelea ni vema amuite katika meza ya majadiliano ya amani, kwa kutaraji kuwa yeye ana upeo wa kuona mbali kuliko viongozi waliomtangulia. Kwa kuuitika na kuukubali kwake wito huu wa amani, alikuwa ameiokoa kaumu yake kutokana na moto wa vita uliowaunguza. Mtume akampelekea ujumbe wa watu thelathini ukiongozwa na Abdullah Ibn Rawaahah-Allah awawiye radhi. Ujumbe huu ukamuendea Useir katika utawala wake Khaybar, wakamwambia: "Je, unatupa amani ili tukuelezee lililotuleta?", akajibu: "Naam, nami nimepata amani kutoka kwenu?". Wakajibu: "Naam", kisha ndipo walipomsihi aachane na azma ya vita aliyoiweka na kwamba aende kwa Mtume wa Allah Madinah. Huko ataapishwa na kutawazwa rasmi uongozi wa Khaybar, ili watu wake wapate kuishi kwa amani na waislamu. Mwanzoni akaonyesha kuuitika wito huu wa amani, akatoka pamoja na waislamu akiongozana na watu thelathini, akimkusudia Mtume Madinah. Alipokuwa njiani akajuta na kujilaumu kwa nini amechukua uamuzi huo wa kumfuata Mtume, akajiwa na fikra za kuwafanyia usaliti watu aliopeana nao amani. Akaurukia upanga wa Abdullah akitaka kumpokonya na kumuua kwa kuutumia, Abdullah akalitambua hilo na kumwambia: "Unataka kufanya usaliti ewe adui ya Allah?". Akamshukia na kumpiga kwa upanga pigo lililo litenganisha paja na muundi wake. Akaanguka kutoka juu ya ngamia wake na hakuchukua muda mrefu akafa kutokana na kutokwa na damu nyingi. Hapo waislamu wakawaendea watu wake walioongozana nao, wakapambana nao na kufanikiwa kuwaua wote.

 

IV.            Mayahudi waazimia kuushambulia mji wa Madinah, Mtume wa Allah awawahi na kuwashambulia kwao:

         Sallaam Ibn Miksham aliposhika hatamu za uongozi wa Mayahudi wa Khaybar baada ya kuuawa kwa Useir Ibn Razaam. Sera yake ilikuwa ni kuendeleza mapambano dhidi ya waislamu kama ilivyokuwa kwa watangulizi wake. Namna hivi ndivyo Mayahudi walivyoendelea kuwa na dhamira ya vita, wakipanga njama za kuwaangamiza waislamu kila kukicha. Wakiazimia kuutokomelezea mbali Uislamu kwa gharama yo yote imkinikayo. Ilipotimia suluhu ya Hudaybiyah baina ya Mtume wa Allah na Makureishi na wakakukbaliana kusitisha vita kwaa muda. Mayahudi wakakata tamaa kupata msaada wa uungaji mkono wa Waarabu katika kuitekeleza azma na dhamira yao hii chafu. Sallaam akawatangazia wazi viongozi wa Khaybar kwamba kuna hatari dhahiri inayotishia uwepo wa Mayahudi Madinah. Na akawaambia kuwa wajibu wao katika kukielekea kitisho hicho ni kuunda kikosi miongoni mwao kwa kushirikiana na Mayahudi wa Waadil-Quraa na Taymaa. Kisha wasonge mbele kuelekea Madinah kuwasagasaga waislamu bila ya kutegemea msaada wa makabila ya Kiarabu katika vita hivi.

Tayari Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa amekwishaijua dhamira hii ya Mayahudi wa Khaybar. Akaanza haraka kuchukua hatua za maandalizi ya vita dhidi yao huko huko kwao kabla hawajatoka kuja Madinah. Miongoni mwa mbinu alizozitumia Bwana Mtume katika kukabiliana na adui yake ni kumshtukiza adui kabla hajashambuliwa yeye ghafla. Lakini mpango na mkakati huu Mtume wa Allah ulivuja, kwani Abdullah Ibn Ubayyi - kama wasemavyo baadhi ya wapokezi - aliwatumia ujumbe Mayahudi wa Khaybar na kuwaambia: "Muhammad huyoo anakujieni kwa hivyo chukueni hadhari yenu". Khabari hii ilipowafikia wakaanza kufanya maandalizi kabambe ya kukabiliana na Mtume waliyeambiwa kuwa anakuja. Wakawa kila siku wakitoka nje ya mji kiasi cha wapiganaji alfu kumi kwa lengo la kumfagilia Mtume huko huko kabla hajaingia mjini kwao. Walitoka wakiwa katika maandalizi ya tayari kwa lo lote, wakiwa na silaha zao, wakawa wanasema: "Muhammad atupige sisi?! Li mbali hilo mno, li mbali mno hilo!" Wakazitia ngomeni mali na familia zao katika ngome za "Kutaybah" na askari wakakusanywa katika ngome za "Nitwaah".

 



 | Tuandikie |