Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

IV. MAZINGIRA YA VITA KATIKA ARDHI YA KHAYBAR

 Faida

            Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaanza vita kwa mtindo wa mzonge akielekeza mashambulizi makali karibu kabisa na ngome ya adui. Mayahudi nao wakipigana kufa kupona kuilinda kila shubiri ya ardhi yao, hawarejei nyuma na kuiacha ardhi yao mateka mikononi mwa waislamu ila kwa kuzidiwa mno. Kila walipojaribu kutoka ngomeni waislamu waliwashushia kisago cha nguvu, wakawa hawana hila ila kurudi kimgongomgongo ngomeni mwao kujipatia  hifadhi na kujipanga upya. Mzingiro ukaendelea kwa siku kadhaa na mapambano yakizidi kupamba moto mpaka waislamu wakakimwa na hali hiyo. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akakaa siku saba akipambana na watu wa ngome hii. Kila siku akimpa bendera ya vita mmojawapo wa maswahaba wake na kumtuma kwenda kushambulia huko ngomeni, lakini akirudi bila ya kupatikana ushindi. Hali ikawa hiyo mpaka pale Allah Taala alipoifungua ngome hiyo kwa mikono ya Sayyidina Aliy Ibn Abi Twaalib-Allah amuwiye radhi.

Katika mapambano haya yaliyopelekea kutekwa kwa ngome hii, aliuuawa shujaa wa Mayahudi; Marhab. Huyu alikuwa ni shujaa wa mashujaa wa Mayahudi, aliuliwa na Sayyidina Aliy katika mubaraza (mpambano wa wawili wawili). Katika waliouliwa kwenye mpambano huu alikuwemo pia Mahmoud Ibn Maslamah kaka wa Muhammad Ibn Maslamah. Huyu aliuawa kwa kudondoshewa jiwe la kusagia wakati alipokuwa amejiegemeza kwenye ukuta wa ngome akijikinga na joto kali la siku hiyo. Katika kipindi cha mzingiro huu, alikufa kiongozi wa Mayahudi; Salaam Ibn Miksham akiuacha uongozi kutwaliwa na Al-Haarith Ibn Abiy Zaynab.

Ngome hii ya Naaim ilipoangukia mikononi mwa waislamu, Mayahudi wakakimbilia katika ngome iliyokuwa nyuma ya ngome hii. Hiyo ndio iliyokuwa ngome ya As-swa’ab Ibn Muaadh, wakajipanga tena humo na kutoa upinzani mkali na wa nguvu kwa waislamu. Wakawaendesha mbio waislamu kama simba aliyejeruhiwa mpaka wakafanikiwa kwa kiasi kikubwa kuvuruga mpango wa mashambulizi wa waislamu. Waislamu wakarudishwa nyuma mpaka mahala alipokuwa amesimama Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Al-Habaab Ibn Al-Mundhir-Allah amuwiye radhi-akasimama imara, huku Mtume akiwahimiza na kuwatia ari ya kupigana waislamu, wakasonga mbele tena wakiwa na nguvu mpya. Wakapigana kwa nguvu ya imani mpaka wakafanikiwa kuisambaratisha na kuikata nguvu ya Mayahudi na kuwalazimisha kurudi nyuma na kujifungia ngomeni mwao. Lakini waislamu wakafanikiwa kupenya ndani, humo kazi ikawa ni moja tu kuua na kuchukua mateka mpaka wakaitia mikononi mwao ngome hii ya pili ya Mayahudi.

Katika ngome hii, waislamu walipata shayiri, tende, samli, zeti, asali na vitu vingine vingi. Kabla ya kuiteka ngome hii, waislamu walikuwa wamekumbwa na janga la njaa kiasi cha kulazimika kula nyama za farasi. Walipofanikiwa kuiteka ngome hii na kukuta chakula tele, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akachelea wasije kushughulishwa na ngawira hii wakasahahu mpambano ulio mbele yao. Akamtuma mtu kuwalingania ya kwamba: “Kuleni na walisheni wanyama wenu lakini msibebe”. – Yaani msichukue kitu cho chote kwa ajili ya kupeleka majumbani mwenu.

 

                v.          Mayahudi wamfahamisha Mtume maficho ya wenzao:

          Katika ngome hii waislamu walikuta ndani ya nyumba moja iliyokuwa chini ya ardhi zana kadhaa za kivita. Hizi zilikuwa ni kombeo, vifaru, mavazi ya chuma, majambia na zana nyingine za kivita ambazo ziliwasaidia sana katika vita hivi. Myahudi mmoja aliyetekwa na waislamu katika mzingiro wa ngome ya Naaim ndiye aliyewapa waislamu siri ya ghala hilo la silaha. Huyu alichelea kuuawa na waislamu, ndipo akaomba kwa Mtume-Rehema na Amani zimshukie-amani ya maisha yake na ya familia yake. Mtume akamkubalia, ndipo alipotoboa siri ya mahala zilipohifadhiwa silaha za Mayahudi katika ngome ya As-swa’ab.

Ngome hii ya As-swa’ab Ibn Muaadh nayo ilipotekwa na waislamu, Mayahudi wakakimbilia katika ngome ya Az-zubeir. Hii ndio iliyokuwa ngome madhubuti isiyopenyeka ila kwa taabu na maarifa ya ziada mno, ngome hii ilikuwa kileleni mwa jabali refu. Waislamu wakaitia mzingironi ngome hii kwa muda wa siku tatu na Mayahudi wakiendelea kujificha humo bila ya kutoka. Kukawawia ugumu mno waislamu kuifungua ngome hii mpaka pale Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipoambiwa na mmoja wao kuwa kuna kijito cha maji nyuma ya ngome hiyo. Kijito hiki ndicho kinachoingiza maji ngomeni humo, Mtume akaamuru kuzibwa kwa kijito kile, ili wakiishiwa na akiba ya maji walazimike kutoka nje. Na kweli walipoishiwa na akiba ya maji wakawa hawana njia ila kutoka nje ya ngome, wakapambana kufa kupona mpaka siku hiyo wakauawa waislamu kadhaa na Mayahudi kumi, huku kukiwa na idadi kubwa ya majeruhi kwa pande zote mbili. Waislamu wakajibu mashambulizi haya kwa mbinu ya nguvu ya mtu mmoja mpaka Allah akawapa ushindi wakaiteka na ngome hii. Hii ndio ilikuwa ngome ya mwisho katika eneo hili la Nitwaah, kutekwa kwa ngome hii kukamaanisha kuangukia mikononi mwa waislamu eneo lote la Nitwaah. Mayahudi haoo wakatimkia kwenye eneo la Shiqi, wakaingia katika ngome ya Ubayyi iliyokuwa juu ya jabali lililoitwa “Shamraan”. Waislamu wakaizingira ngome hii na kukumbana na upinzani mkali kutoka kwa Mayahudi. Baada ya mubaraza wa mashujaa wa pande mbili hizi, waislamu wakaivaa ngome hii wakiongozwa na Abu Dujaanah Al-Answaariy mpaka wakafanikiwa kupenya ndani. Wapiganaji wa Kiyahudi waliposhindwa kuhimili nguvu ya waislamu, wakaanza kuparamia kuta kukimbilia kwenye ngome ya Al-Barii. Humo wakachaga na kutoa upinzani mkali mno. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akawaongoza maswahaba wake kuiendea ngome hii. Watu wa ngome hii walikuwa mahiri mno katika utupaji wa mishale na kuvurumisha mawe, wakaachia mvua ya mishale na mawe kiasi cha kumpata Mtume wa Allah. Kutokana na kitisho hiki na mtindo/mbinu hii itumiwayo na Mayahudi, Mtume akaamuru kulengwa kombeo tayari kuisambaratishia mbali ngome hii. Hili likawatia khofu kuu Mayahudi wa ngome hii, wakaisalimisha ngome na kutimua mbio. Kama hivi ndivyo lilivyoangukia mikononi mwa waislamu eneo lote la la Shiqi kama ilivyokuwa kwa eneo la Nitwaah.

Mayahudi sasa wakaelekea katika eneo lao la mwisho; eneo la Kutaybah, wakajitia katika ngome ya Qamuuswi ambayo ni ngome ya Banil-Huqayq. Hii ilikuwa ni miongoni mwa ngome madhubuti mno iliyokuwa chini ya uongozi wa baadhi ya watukufu wa ukoo huu wa Al-Huqayq. Humo ndimo walimowekwa wanawake wa ukoo huu, Mtume na maswahaba wake wakaendeleza wimbi la ushindi kwa kuizingira ngome hii kwa muda wa siku ishirini. Ndipo Allah alipoifungua kupitia mikono ya Sayyidina Aliy Ibn Abi Twaalib-Allah amuwiye radhi na wote maswahaba wa Mtume. Lilichukuliwa mateka katika ngome hii, kundi kubwa la wanawake na watoto, miongoni mwa wanawake hao alikuwemo Bi. Safiyah Bint Huyay. Huyu aliteuliwa na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kuwa mkewe. Akamuacha huru na kumuoan, kwa hivyo akawa miongoni mwa mama wa waumini-Allah awawiye radhi wote.

 



 | Tuandikie |